Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kwa nini baadhi ya majengo huegama bila kuanguka?
Leaning Tower of Pisa ni moja ya alama maarufu zaidi nchini Italia, lakini siyo jengo pekee linaloinama upande mmoja. Kuanzia "Dancing Houses" nchini Uholanzi hadi hekalu la "Tiger Hill" nchini China, majengo yanayoinama yanaweza kupatikana sehemu mbalimbali duniani.
Lakini kwa nini majengo haya huinama? Na kwa nini hali hiyo haimaanishi lazima yataanguka?
Kwa kawaida, majengo huinama kutokana na msingi wake kuzama au kusogea upande mmoja, mara nyingi kwa sababu ya udongo laini, maji chini ya ardhi, au makosa ya ujenzi. Hata hivyo, jengo linaweza kuendelea kusimama ikiwa uzito wake bado unasambazwa vizuri juu ya msingi wake.
Kwa nini baadhi ya majengo huinama?
Kulingana na Dkt. Mandy Korff, Profesa Mshiriki wa Uhandisi wa Miundombinu ya Udongo (Geotechnical Practice) katika Chuo cha Teknolojia, Delft na taasisi ya Deltaes, kuna sababu kadhaa za majengo kuinama upande mmoja.
Katika baadhi ya hali, kama ilivyo kwa "Dancing Houses" nchini Uholanzi, sababu ni aina ya misingi inayotumika wakati wa ujenzi. Misingi hiyo inaweza kufanya jengo liwe na mwendo au mabadiliko madogo ya kimuundo kwa muda, jambo linalosababisha lionekane kama linainama.
End of Unaweza kusoma
Korff anasema: "Katikati ya Amsterdam, nyumba nyingi zilijengwa juu ya nguzo za miti.
Anaeleza kwamba hizi nguzo za msaada huwekwa kwa jozi chini ya kuta na sehemu za mbele za majengo.
Nguzo hizo huingia hadi kina cha takribani mita 12 ndani ya udongo, ambao mara nyingi huwa na udongo laini wa mfinyanzi, mboji au mchanga.
Anasema: "Ikiwa hali iko hivi na nguzo hizo ziko imara, hakuna kitakachotokea kwa nyumba."
Lakini anasema kwamba ikiwa hizi nguzo zitaanza kuharibika au kuoza, nyufa zinaweza kuanza kuonekana, na uharibifu au mgawanyo usio sawa wa uzito unaweza kusababisha majengo kuinama taratibu kadiri muda unavyopita.
Hali ya mnara Pisa kwa sasa bado umeinama
Hali ya udongo pia inaweza kusababisha majengo kuegemea upande mmoja, kama ilivyotokea katika Mnara maarufu wa kuinama wa Pisa.
Profesa Nunziante Squillia, mtaalamu wa mekanika ya udongo na misingi katika Chuo Kikuu cha Pisa, ni sehemu ya timu inayofuatilia mwelekeo wa kuegemea kwa mnara huo.
"Mnara ulianza kuegemea tangu mwanzo wa ujenzi wake kutokana na udongo kuwa laini sana," Squealilla aliiambia makala ya BBC, Witness History. "Ulishuka kati ya mita tatu na nne."
Majengo pia yanaweza kuegemea kutokana na mabadiliko ya udongo yanayosababishwa na binadamu, kwa mfano mnara wa kanisa la "Ode Kirk", au Kanisa la Kale, huko Delft.
Korf anasema: "Hili halijulikani sana, lakini linakaa kwa njia inayofanana kwa kiasi fulani na kuegemea kwa Mnara wa Pisa."
Anaongeza: "Umeegemea kuelekea mfereji wa maji kwa sababu udongo upande mmoja ulichimbwa ili kutengeneza mfereji huo, na upande huo umekuwa laini kuliko upande mwingine. Kwa hiyo kuna shinikizo kidogo la kuuweka wima, na kisha walipojenga, ulianza kuegemea."
Mabadiliko katika maji ya chini ya ardhi pia yanaweza kusababisha majengo kuegemea upande mmoja. Na wakati mwingine, kama Korff anavyoeleza, majengo hujengwa yakiwa yameegemezwa kwa makusudi.
Anasema: "Nyumba nyingi huko Amsterdam zilijengwa zikiwa zimeegemea mbele, kwa sababu hiyo ndiyo ilikuwa namna ya kujenga nyumba za wafanyabiashara zamani."
Anaongeza: "Mara nyingi zilijengwa kando ya mifereji ya maji kwa ajili ya kuhifadhi bidhaa, na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kuingia ndani ya nyumba, kwa hiyo zilijengwa zikiwa zimeegemea mbele. Hivyo, ikiwa imeegemea mbele, haimaanishi kuna tatizo. Lakini inapoegemea upande, unajua kwa uhakika kwamba haikukusudiwa hivyo."
Ukarabati
Kwa hiyo, pamoja na majengo haya yote yanayoegemea, kwa nini hatuoni hilo kama tatizo kubwa?
Kulingana na Dkt. Korff, kuegemea kwa jengo si lazima kumaanishe kuwa jengo hilo haliko imara kimuundo.
Anasema: "Mwelekeo wa kuegemea lazima uwe mkubwa sana ndipo jengo liwe na kuyumba kimuundo."
Lakini wakati mwingine mwelekeo huo lazima usahihishwe, kama ilivyotokea katika Mnara wa Kuegemea wa Pisa.
Ingawa mnara huo ulianza kuegemea mapema sana wakati wa ujenzi wake, vipimo vilionesha kuwa hali ilizidi kuwa mbaya katika karne ya ishirini, ambapo kuegemea kwake kuliongezeka taratibu.
"Hali ilikuwa ya kutia wasiwasi sana," anasema Squellia.
Kisha mwaka 1989, mnara wa kiraia katika mji wa Pavia nchini Italia ulianguka. Kulingana na Squillia, tukio hilo lilikuwa "kichocheo," na Mnara wa Pisa kufungwa mwaka uliofuata.
Kulikuwa na mawazo mengi kuhusu jinsi ya kunyoosha tena mnara huo uliokuwa umeegemea kidogo ili kuufanya uwe salama tena.
"Mbinu iliyochaguliwa ilikuwa ni kuondoa udongo," anasema Squellia.
Anaongeza: "Bila kugusa mnara wenyewe, mita za ujazo 37 za udongo ziliondolewa upande wa kaskazini wa misingi yake."
Mnara huo ulifunguliwa tena baada ya miaka 11.
Korff anasema inawezekana kurekebisha mwelekeo wa jengo kwa kulinyanyua kwa kutumia korongo, kama vile gari linavyoweza kunyanyuliwa, lakini wakati mwingine hilo linaweza kuleta madhara zaidi kuliko faida.
Anaongeza: "Kama jengo limeegemea kweli, ni hatari pia kulirudisha katika hali ya wima, kwa sababu jengo huwa tayari limezoea hali yake ya kuegemea."
Anasema: "Lazima uwe makini sana, angalau ili usizidishe tatizo."
Ingawa baadhi ya majengo yanaweza kuimarishwa na kutengemaa, hilo pia lina changamoto zake.
Korf anasema: "Wanaweza kufanya mambo mbalimbali na majengo, chochote kinawezekana."
Anaongeza: "Lakini inagharimu pesa nyingi na ni jambo gumu."
Athari ya mabadiliko ya tabia nchi
Utafiti wa Korff uligundua kuwa kuna takribani nyumba 75,000 nchini Uholanzi pekee zilizojengwa juu ya nguzo za mbao na ziko katika hatari ya kuharibika, huku karibu mara tatu ya idadi hiyo zikikabiliwa na hatari hiyo kutokana na misingi isiyo na kina kirefu.
Matatizo haya huenda yakazidi kuwa mabaya zaidi.
Korff anasema: "Pamoja na mabadiliko ya tabianchi na mabadiliko katika maji ya chini ya ardhi, wakati mwingine tunaona mabadiliko ya haraka zaidi."
Kiwango cha maji ya chini ya ardhi kikishuka, misingi ya mbao huonekana wazi, jambo ambalo linaweza kuharakisha kuharibika kwake. Mabadiliko katika maji ya chini ya ardhi pia yanaweza kuathiri tabaka za udongo, ambalo kwa upande wake huathiri nyumba zilizo na aina mbalimbali za misingi.
Hata hivyo, aliongeza kuwa mchakato huo hutokea taratibu.
Kuhusu Mnara wa Kuegemea wa Pisa, kuegemea kwake kulipunguzwa kwa zaidi ya sentimita 40 baada ya miaka 11 ya kazi iliyokamilika mwaka 2001. Wahandisi wanaamini kuwa mustakabali wake uko salama kwa angalau miaka 200 ijayo.