Mwanaume aliyetangazwa kufa na kuzikwa arudi nyumbani baada ya siku moja

Muda wa kusoma: Dakika 4

Wakaazi wa Manispaa ya Masindi waliachwa na mshangao baada ya mwanaume aliyetangazwa kuwa amekufa kurudi akiwa hai, saa chache tu baada ya mwili unaoaminika kuwa wake kuzikwa.

Kwa mujibu wa mtandao wa Daily Monitor, Godwin Baguma, mkazi wa Kijana wa Kijura katika Kitengo cha Kati, nchini Uganda aliripotiwa kutoweka wiki kadhaa, na kusababisha wasiwasi miongoni mwa wanafamilia na majirani.

Kulingana na familia, Baguma, ambaye anasemekana kuwa na tatizo la afya ya akili, alitoweka bila kumjulisha mtu yeyote, na kusababisha msako mkali.

Hali ilibadilika mwishoni mwa wiki wakati familia ilipopokea taarifa kwamba polisi wameupata mwili uliokuwa umeoza kutoka kwenye shamba la miwa katika huko Kisanja siku ya Ijumaa.

Mwili ulipelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Masindi, ambapo matangazo yalitolewa kwa watu wenye watu waliopotea ili kusaidia katika utambuzi.

Baba yake Baguma, Yakobo Kamuturaki, alisema baada ya kupokea taarifa siku ya Jumapili, aliwatuma wanawe kwenda kwenye chumba cha kuhifadhia maiti ili kuthibitisha kama mwili huo ni wa mwanawe aliyepotea. Baada ya kutazama mabaki, walirudi na kuthibitisha kuwa ni wa Baguma.

Mazishi yafanyika

"Tuliambiwa mwili ulikuwa katika hali mbaya. Wanangu walikwenda na kuutambua kuwa ni wa kaka yao. Tuliwaamini na kukubali kwamba amekufa," Kamuturaki alisema.

Kufuatia uthibitisho huu, familia ilipanga mipango ya mazishi haraka kutokana na kuoza. Habari za kifo cha Baguma zilienea haraka huko Kijura na maeneo ya jirani, na kuwavutia waombolezaji nyumbani.

Mazishi yalifanyika Jumapili, huku familia ikipanga kufanya ibada ya mwisho ya mazishi siku iliyofuata [Jumatatu].

Hata hivyo, kile kilichoanza kama maombolezo mazito kiligeuka maajabu na kuchanganyikiwa. Wakati maandalizi ya ibada ya mwisho yakiendelea Jumatatu, ripoti zilianza kusambaa kwamba Baguma ameonekana akiwa hai katika kijiji cha Kihanguzi katika Kaunti Ndogo ya Labongo, Wilaya ya Masindi.

"Mwanzoni, tulipuuza uvumi huo. Tayari tulikuwa tumezika mwili. Lakini tuliamua kwenda kuthibitisha." Dada yake Baguma, Jane Birungi alisema.

Alisema wanafamilia walikimbilia eneo hilo, na wakamkuta Baguma akiwa hai. Inaripotiwa kwamba alikuwa amelala nyumbani kwa rafiki yake.

"Tulipomwona, tulishtuka. Hatukuweza kuamini ni yeye akiwa hai," anasema Birungi.

Baguma alirudishwa nyumbani mara moja, na kusimamisha shughuli za msiba zilizokuwa zikiendelea.

Kufukua mwili

Tukio hilo huo lililazimisha familia hiyo kuingia katika mchakato mgumu wa kufukua mwili ambao tayari ulikuwa umezikwa. Mabaki hayo, ambayo awali yaliaminika kuwa ya Baguma, sasa yanashukiwa kuwa ya mtu asiyejulikana.

"Tayari tulikuwa tumeomboleza na hata kuzika mwili huo. Kisha ghafla, mtu tuliyemdhania amekufa anarudi akiwa hai. Hili ni jambo ambalo hatujawahi kushuhudia hapo awali," Bi Janet Asiimwe, jirani alisema.

Mkazi mwingine, Bi Florence Bikorwa, alielezea tukio hilo kama la ajabu ambalo hajawahi kushuhudia katika maisha yake yote.

"Ni kama filamu. Watu walichanganyikiwa na kuogopa. Hakuna mtu aliyeweza kuelewa kinachoendelea," alisema.

Polisi wamethibitisha tukio hilo na kuanzisha uchunguzi ili kubaini utambulisho wa mwili uliozikwa kimakosa.

Solomon Mugisa, Afisa wa Uhusiano wa Jamii wa Mkoa wa Albertine Kaskazini na kaimu msemaji wa polisi, alisema mwili huo ulipatikana Ijumaa iliyopita na kupelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti.

"Familia ilikuja na kutambua mwili huo kama ndugu yao na kuanza mipango ya mazishi. Baadaye, waligundua kuwa jamaa yao alikuwa hai, jambo lililosababisha mkanganyiko," Mugisa alisema.

Aliongeza hilo lilisababisha kufukuliwa kwa mwili huo na kurejeshwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Masindi.

Polisi wamewahimiza umma kuwa waangalifu wanapotambua miili, hasa ile iliyooza.

"Katika hali kama hizo, utambuzi lazima ufanyike kwa uangalifu, na familia zinapaswa kufanya kazi kwa karibu na wafanyakazi wa matibabu ili kuepuka makosa kama hayo," Mugisa alishauri.

Pia alisisitiza kwamba taratibu sahihi za kisheria lazima zifuatwe wakati wa ufukuaji wa maiti, ikiwa ni pamoja na kupata amri ya mahakama, mapendekezo kutoka mamlaka za mitaa, na ushiriki wa polisi.