Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Nadharia tatu kuhusu uwezekano wa kutokea mwisho wa dunia
Mwisho wenye baridi, wenye giza, na kwa kiasi fulani wa huzuni. Mwisho wa vurugu na maangamizi makubwa. Au labda mwisho ambao ndani yake umebeba mwanzo mwingine?
Hizi ni baadhi ya nadharia maarufu kuhusu jinsi mwisho wa dunia au ulimwengu unaweza kuwa katika siku za mbali sana zijazo, ikiwa kweli kutakuwa na mwisho kabisa.
Hatima ya ulimwengu ni mojawapo ya maswali yenye siri kubwa zaidi katika sayansi. Hata wanasayansi wanaamini kwamba kuna maswali mengi kuliko majibu.
Ili kuelewa baadhi ya njia ambazo ulimwengu unaweza kufikia mwisho wake, kwanza tunahitaji kuelewa jinsi ulimwengu ulivyoanza.
Mwanzo wa kila kitu
Kulingana na NASA, ulimwengu ni kila kitu: anga lote, vitu vyote vya maada (chochote kinachochukua nafasi na kuwa na uzito), nishati, na hata muda wenyewe.
Jinsi ulimwengu ulivyotokea inaelezewa na kile ambacho wanaastronomia wanakiita nadharia ya "Big Bang."
Nadharia hii inasema kwamba takribani miaka bilioni 13.8 iliyopita, ulimwengu ulikuwa katika hali ya joto kali sana na yenye msongamano mkubwa, na tangu wakati huo umekuwa ukitanuka mfululizo.
Ulimwengu umeendelea kupanuka, na baada ya kipindi kirefu sana cha muda, miundo kama vile galaksi, nyota, na sayari iliundwa.
Mchakato wa kupanuka kwa ulimwengu bado unaendelea hadi sasa.
Lakini kimsingi tunajua mambo machache sana kuhusu ulimwengu.
"Kazi yetu ni kama kutazama tabia na mtiririko wa mto mzima bila kuwa na uwezo wa kuchunguza kikamilifu molekuli zote za maji zinazopita ndani yake," anasema Alexandre Zabot, mwanafizikia katika Chuo cha Santa Catarina nchini Brazil.
Nadharia ya 'Big Freeze'
Taasisi ya Royal Observatory Greenwich nchini Uingereza inasema kwamba ikiwa ulimwengu utaendelea kupanuka, nishati yake itatawanyika sana kiasi kwamba galaksi zitaendelea kusogea mbali zaidi kutoka kwa nyingine. Hatimaye, nyota mpya hazitazaliwa tena, na nyota zilizopo zitazimika.
Hali hii inajulikana kama "Big Freeze" au "Heat Death of the Universe" (Kifo cha Ulimwengu).
Kulingana na taasisi hiyo, mtazamo huu unasema kwamba mwishowe atomi zote katika ulimwengu zitafikia thermal equilibrium, yaani, hali ambapo joto litakuwa sawa kila mahali. Matokeo yake, karibu kila kitu kitaacha kusogea na kubadilika.
Kwa mujibu wa nadharia hii, siku moja joto kila sehemu ya ulimwengu litakuwa sawa, na baada ya hapo kila kitu kitaanza kusimama polepole.
Nadharia hii inaeleza kwamba atomi zote katika ulimwengu zitafikia usawa wa joto, na kila kitu kitapoteza nguvu ya kuendelea kufanya kazi au kubadilika.
"Kila kitu kinaonesha kwamba ulimwengu utakuwa tupu zaidi, baridi zaidi, na wenye umbali mkubwa zaidi kati ya vitu," anasema Raul Abramo wa Taasisi ya Fizikia katika Chuo cha São Paulo nchini Brazil. "Galaksi zinaendelea kutengana zaidi na zaidi, na nyota zinachakaa na kufa. Hii ndiyo hali ya mwisho ambapo ulimwengu utakuwa kama makaburi makubwa."
Ukungu unaotoweka
Ikiwa hali hii si ya kufurahisha sana, kuna nadharia nyingine; ingawa matokeo yake yanaweza kuwa makali zaidi.
Kama inavyoelezwa na Royal Museums Greenwich, nadharia hii inategemea wazo kwamba ulimwengu unapanuka kwa kasi inayoongezeka, ikisukumwa na kitu kinachoitwa nishati ya giza.
Ikiwa hali hii itaendelea, upanuzi wa ulimwengu unaweza kuwa wa kasi sana kiasi kwamba nguvu ya mvutano haiwezi tena kushikilia miundo ya vitu pamoja.
Dhana hii inajulikana kama Big Rip, kupasuka kwa kiasi kikubwa.
NASA inaeleza: " nguvu ya mvutano ni nguvu inayosababisha sayari au kitu kingine kuvuta vitu kuelekea katikati."
Mvutano hushikilia sayari kwenye mzunguko wa jua, hushikilia Dunia mahali pake, na huzuia wanadamu kutawanyika angani. Ni nguvu inayoshikilia mifumo kama nyota, mifumo ya jua, galaksi, na makundi ya galaksi pamoja.
Kwa upande mwingine, nishati ya giza ni kitu kisichoeleweka vizuri na inaonekana kuwa na athari ya kinyume kabisa. "Bado hatujui imetengenezwa na nini, lakini tunajua husababisha aina ya msukumo unaofanana na 'antigravity,'" anaeleza Alexandre Zabot.
Kulingana na NASA, nishati ya giza ndiyo inayosababisha ulimwengu kupanuka kwa kasi inayoongezeka. Shirika hilo linasema takribani asilimia 68.3 hadi 70 ya ulimwengu mzima inaundwa na nishati ya giza.
Hali hii iligunduliwa kwa mara ya kwanza mwishoni mwa miaka ya 1990.
Kwa muda mrefu jambo hili halikujulikana kwa sababu kwa kiwango cha maisha ya binadamu, sayari, au hata galaksi, nguvu ya mvuto huificha athari yake. Nishati ya giza huonekana tu katika viwango vikubwa sana, katika umbali kati ya galaksi.
Kulingana na Profesa Zabot, kadiri ulimwengu unavyozidi kupanuka, athari ya kusukuma ya nishati ya giza pia huongezeka, na huenda kadiri ulimwengu unavyokuwa mkubwa zaidi, athari yake ikaanza kuonekana hata katika viwango vidogo zaidi.
NASA inasema kutokuwa na utulivu kwa nishati ya giza kunaweza kusababisha "Big Rip", hali ambapo upanuzi wa ulimwengu unakuwa mkali kiasi kwamba miundo yote ya ulimwengu, kuanzia nyota hadi atomi, husambaratika.
"Hivyo ndiyo maana jina la nadharia hii lina pande mbili," anasema Zabot. "Inaitwa 'Big Rip,' neno linalomaanisha mgawanyiko, mpasuko, au kuvunjika kwa nguvu."
Anaongeza: "Wakati huohuo, neno hilohilo kwa ufupisho wake linaweza pia kumaanisha jambo linalohusiana na furaha ya nafsi."
Kuna uwezekano mwingine wa kati ambao pia ni wa kutisha.
Ikiwa nishati ya giza itadhoofika au hatimaye kubadilisha mwelekeo wake, mvuto unaweza kuanza kuvuta ulimwengu wote kurudi pamoja.
NASA inasema kwamba hali hii inaweza kusababisha ulimwengu kukusanyika tena na hatimaye kuanguka, na katika baadhi ya maelezo ya kinadharia, huweza kuhusishwa na mchakato unaoishia katika hali ya msongamano mkali sana kama ulivyokuwa mwanzoni mwa 'Big Bang'.
Nadharia nyingine inasema kwamba ulimwengu unaweza kuanguka tena kwa mara moja, kisha "Big Bang" nyingine ikatokea, na kuunda ulimwengu mpya.
Dhana hii wakati mwingine hujulikana kama 'Big Bounce', ambayo inaeleza kwamba ulimwengu unaweza kupitia mizunguko isiyo na mwisho ya kukandamizwa, kubanwa, kupanuka, na kupanuka tena.
Lakini kama anavyosema Raul Abramo, "Huu ni mtindo wa kushangaza ambao hatuna taarifa wala ushahidi wa moja kwa moja kuuthibitisha."
Kwa hiyo, je, inawezekana kukisia ni lini ulimwengu utafikia mwisho wake?
"Hapana, hatuna dalili wala ushahidi kwamba kutakuwa na mpasuko mkubwa au kuanguka kwa ulimwengu katika siku zijazo," anaeleza Raul Abramo.
"Baadhi ya makadirio yanaonesha kwamba mwisho huo unaweza kutokea katika kipindi cha mabilioni mengi sana ya miaka ijayo, huku wengine wakiamini kuwa utachukua muda mrefu zaidi," anaongeza Alexandre Zabot.
Ikiwa ulimwengu una angalau miaka bilioni 13.8 ya umri, bado kuna muda mrefu sana kabla ya kufikia hata trilioni moja ya miaka.
Utafiti mpya kutoka Radboud University nchini Uholanzi unapendekeza kwamba ulimwengu unaweza kuwa unaharibika na kupungua kwa kasi zaidi kuliko ilivyodhaniwa hapo awali. Watafiti wamekadiria kwamba mabaki ya mwisho ya nyota yanaweza kutoweka baada ya takribani miaka "kumi hadi nguvu ya sabini na nane" yaani namba 1 ikifuatiwa na sufuri 78.
Huenda hakutakuwa tena na viumbe vya aina yoyote duniani vitakavyoshuhudia mwisho huo.
Dunia yenyewe inaweza kuwa ilitoweka muda mrefu kabla ya hapo, wakati ambapo Jua linatarajiwa kugeuka kuwa nyota kubwa nyekundu, jambo ambalo linakadiriwa kutokea baada ya takribani miaka bilioni sita ijayo.
"Ukweli ni kwamba bado tunajua mambo machache sana kuhusu kosmolojia," anasema Profesa Abramo. "Vifaa tulivyo navyo leo vina mipaka, jambo linalofanya iwe vigumu kufanya vipimo sahihi vya ulimwengu."
Na hali hiyo ndiyo inayofungua nafasi ya kuchunguza na kupendekeza nadharia mbalimbali za kubuni au za kufikirika, kama vile dhana ya multiverse au ulimwengu sambamba , ambazo zinapendekeza kuwepo kwa zaidi ya ulimwengu mmoja.