Kiongozi Mkuu wa Iran amesema kuwa Marekani na Israel wanajaribu “kuidhibiti” nchi yake
Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Mojtaba Khamenei, amesema siku ya Alhamisi katika ujumbe wa maandishi uliosomwa kwenye televisheni ya serikali kuwa Marekani na Israel wanajaribu kuiyumbisha Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Ayatollah Mojtaba Khamenei, ambaye hajaonekana hadharani tangu alipoingia madarakani Machi mwaka jana, aliongeza kusema: “Mpango huo wa adui, baada ya vita vilivyolazimishwa, shinikizo la kiuchumi na kizuizi cha kisiasa na vyombo vya habari, ni kuleta migawanyiko na kusambaratika ili kufidia kushindwa kijeshi na kuinyong'onyeza Iran.”
Haya yanajiri baada ya Jeshi la Mapinduzi la Iran kutangaza kuwa walilenga kituo cha kijeshi cha Marekani kujibu mashambulizi ya Marekani kusini mwa nchi hiyo, kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Iran.
Taarifa ya jeshi, iliyoripotiwa na televisheni ya Iran, ilisema: “Kufuatia shambulio lililofanywa asubuhi hii na jeshi la Marekani dhidi ya eneo karibu na uwanja wa ndege wa Bandar Abbas kwa kutumia mabomu ya angani, saa 4:50 asubuhi (01:20 GMT) kituo cha kitengo cha anga cha Marekani kilichokuwa chanzo cha shambulio hilo kililengwa.”
Hakukuwa na maelezo ya wazi kuhusu eneo la kambi hiyo, lakini Kuwait, mshirika wa Marekani, ilitangaza asubuhi ya Alhamisi kuwa ilifanikiwa kudhibiti mashambulizi ya makombora na droni.
Kuwait imekemea kile ilichokiita “mashambulizi ya kikatili ya Iran” yaliyolenga eneo lake, ikisema ni “ongezeko hatari la mivutano na ukiukaji wa wazi wa mamlaka yake, usalama na uadilifu wa eneo lake, pamoja na tishio la moja kwa moja kwa maisha ya raia na miundombinu muhimu,” kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Kuwait.
Wizara hiyo ilisema katika taarifa yake kwamba “ongezeko hilo la mivutano linakuja wakati juhudi kubwa zinaendelea kufanywa… kupunguza mvutano na kutuliza hali na kuzuia eneo hilo kuingia katika mzunguko mpya wa migogoro, jambo linaloongeza uzito wa mashambulizi haya na kudhoofisha juhudi za kidiplomasia za kulinda usalama na utulivu wa kikanda,” na ikaishinikiza Iran “ikomeshe mara moja na bila masharti mashambulizi haya ya kikatili na kubeba jukumu kwa matendo hayo.”
Unaweza kusoma;