Moja kwa moja, Marekani yaishambulia Iran mara ya pili ndani ya siku tatu

Iran imeyalaani mashambulizi hayo na kuyataja kuwa “ukiukaji mkubwa wa usitishaji mapigano”, huku ikionya kuwa haitaliacha “tendo lolote la uhasama bila majibu.”

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Marekani yaanzisha kituo cha afya Kenya kuwahifadhi Wamarekani waliokumbwa na Ebola

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Japokuwa wizara ya afya ya Kenya ilikanusha kuwa imekubali kuweka karantini ya wamarekani walioambukizwa ebola, Ikulu ya Marekani imethibitisha Jumatano kuwa Marekani inaanzisha kituo cha afya nchini Kenya kitakachopokea Wamarekani waliokumbana na virusi vya Ebola katika maeneo yaliyoathirika na mlipuko unaoendelea.

    Kwa mujibu wa afisa wa utawala, Marekani itaanzisha kile alichokiita “kituo cha kisasa kabisa” nchini Kenya kupitia juhudi za pamoja kati ya Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Afya na Huduma za Kibinadamu, na Wizara ya Vita.

    Taarifa hiyo iliripotiwa kwanza na gazeti la The Wall Street Journal.

    Wakati huohuo, Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio amesema katika kikao cha Baraza la Mawaziri Jumatano kuwa serikali “haitaruhusu mtu yeyote aliyeambukizwa Ebola kuingia Marekani.”

    Afisa huyo amesema lengo na muundo wa kituo hicho ni “kutoa huduma bora kwa Wamarekani wanaohitaji kuondolewa haraka” kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ili kuwekwa karantini, akisema hatua hiyo itapunguza “hatari za safari ndefu ya kurejeshwa Marekani.”

    “Wagonjwa wa Ebola wanahitaji huduma kwa haraka, na kituo hiki kitawawezesha Wamarekani walioko eneo hilo wanaoambukizwa Ebola kupata huduma za kuokoa maisha haraka iwezekanavyo bila safari ya zaidi ya saa 12 ya ndege ya uokoaji wa kimatibabu,” amesema afisa huyo.

    Ameongeza kuwa uwezo wa matibabu katika kituo hicho cha Kenya unatarajiwa kushughulikia “aina zote za ugonjwa wa Ebola, ikiwemo huduma za wagonjwa mahututi,” lakini akaeleza kuwa wagonjwa watatathminiwa mmoja mmoja ili kuamua kama wanahitaji kuhamishwa kwenda vituo vingine vyenye huduma za juu zaidi.

    Rubio pia amesisitiza dhamira ya serikali yake ya kudhibiti Ebola, akisema kuwa “kipaumbele cha kwanza cha sera yetu ya mambo ya nje ni kulinda raia wa Marekani.”

    “Haturuhusu na hatutaruhusu mtu yoyote aliyeambukizwa Ebola kuingia Marekani,” amesema Rubio, akiongeza kuwa “mashirika mbalimbali ya serikali” yanahusika na “kufuatilia watu ili kuhakikisha hakuna anayeingia nchini akiwa na Ebola na kusababisha tatizo,” akisema hatua hizo zinaendelea vizuri.

    Serikali ya Marekani hapo awali ilitumia mamlaka yake chini ya kifungu cha Title 42 kuzuia safari za kuingia Marekani kwa wasio raia, isipokuwa baadhi, waliotembelea DRC, Uganda au Sudan Kusini ndani ya siku 21 zilizopita. Amri hiyo ilipanuliwa wiki iliyopita kujumuisha pia wenye kadi za ukaazi wa kudumu (green card).

    Raia wa Marekani waliotembelea nchi hizo wanaelekezwa kupitia viwanja maalum vya ndege kwa uchunguzi wa ziada wa afya, vikiwemo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dulles, John F. Kennedy New York, Hartsfield Jackson Atlanta, na George Bush Intercontinental Houston.

  2. Kenya: Mwongozo wa usalama wa shule mwaka wa 2008

    Serikali ya Kenya ilitoa mwongozo mpya mwaka wa 2008 kuhusu usalama shuleni, kufuatia ghasia zilizotokea nchini humo karibu na uchaguzi wa 2007.

    Ilijumuisha itifaki za usalama wa mabweni, ikiwa ni pamoja na sheria zinazosema kwamba kila bweni linapaswa kuwa na mlango kila eneo la mwisho na njia ya dharura ya ziada katikati.

    Sheria hiyo ni pamoja na kwamba madirisha ya mabweni yanapaswa kuwa bila vyuma na "lazima iwe rahisi kufungua nje". Pia inasema kuwa vifaa vya kuzima moto "vinapaswa kufanya kazi na kuwekwa katika kila njia ya kutoka na ving'ora vya moto vilivyowekwa kwenye sehemu zinazofikika kwa urahisi".

  3. Wanafunzi kadhaa wahofiwa kufariki katika moto wa bweni la shule Gilgil Kenya

    h

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Ni picha ya awali ya tukio jingine lililofanyika mwaka jana

    Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya limesema limefika kwa tukio la moto ulioteketeza bweni katika Chuo cha Wasichana Utumishi kilichopo Gilgil, Kaunti ya Nakuru, ambapo kuna hofu kuwa wanafunzi kadhaa wamepoteza maisha.

    Taarifa zinasema moto huo ulianza majira ya saa saba usiku (1:00 usiku) na kuripotiwa takriban saa tisa na nusu usiku (3:30 usiku) Alhamisi, kwa mujibu wa Msalaba Mwekundu Kenya.

    Katika taarifa yake, shirika hilo limesema:

    “Baada ya tukio la moto lililoripotiwa saa 3:30 usiku katika Chuo cha Wasichana Utumishi, Kaunti ya Nakuru, Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya umefika kusaidia katika operesheni ya dharura inayoendelea.”

    Limeongeza kuwa:

    “Wahudumu wetu wa kwanza, kikosi cha ambulensi cha EMS Kenya pamoja na wataalamu wetu wa usaidizi wa kisaikolojia wako eneo la tukio kuwasaidia wanafunzi walioathirika pamoja na wahudumu wengine na mamlaka husika.”

    Shughuli za uokoaji na tathmini ya tukio hilo bado zinaendelea huku mamlaka zikichunguza chanzo cha moto huo.

    Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Bonde la Ufa, Samuel Ndanyi, amesema kuna wanafunzi wasiopungua kumi ambao bado hawajulikani walipo.

    “Timu zetu zipo eneo la tukio kukusanya taarifa zaidi na kuwabaini wanafunzi wote kama sehemu ya uchunguzi wa tukio hili. Tuna vifo na ni muhimu familia ziarifiwe kwanza,” alisema.

    Wazazi wamefurika katika lango la shule baada ya taarifa za tukio hilo kusambaa Gilgil na maeneo jirani, huku polisi wakizuia idadi kubwa kuingia ndani ya shule na kuruhusu wazazi pekee wakati shughuli za uokoaji zikiendelea.

    Wanafunzi waliojeruhiwa wamekimbizwa katika Hospitali ya St. Joseph’s Gilgil kwa matibabu na uchunguzi zaidi.

  4. Marekani yaishambulia Iran mara ya pili ndani ya siku tatu

    f

    Chanzo cha picha, US Navy via Getty Images

    Jeshi la Marekani limetekeleza mashambulizi mapya dhidi ya Iran, likilenga eneo la kijeshi katika mji wa kimkakati wa bandarini wa Bandar Abbas.

    Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani katika Mashariki ya Kati (Centcom) imesema vikosi vyake pia vilidungua droni nne za mashambulizi za Iran ambazo “zilikuwa tishio katika eneo la Mlango wa Hormuz”.

    Kwa mujibu wa Centcom, eneo lililoko Bandar Abbas lilishambuliwa wakati likiwa linajiandaa kurusha droni ya tano. Vyombo vya habari vya Iran viliripoti kuwa milipuko ilisikiwa mashariki mwa mji huo.

    Mashambulizi hayo yanakuja wakati wa usitishaji mapigano wenye hali tete kati ya Marekani na Iran, pamoja na mazungumzo yanayoendelea ya kumaliza vita vya miezi mitatu vilivyosababisha usafiri wa meli katika Mlango wa Hormuz kuvurugika na bei za nishati duniani kupanda kwa kasi.

    Hii ni mara ya pili ndani ya siku tatu kwa Marekani kushambulia maeneo nchini Iran, huku ikisema mashambulizi hayo yalifanywa kwa kujilinda.

    Mashambulizi hayo mapya yanaongeza hofu ya kuvunjika kwa usitishaji mapigano uliopo.

    Centcom ilieleza hatua zake kuwa “za tahadhari, za kujihami pekee, na zinazolenga kudumisha usitishaji mapigano.”

    Mapema wiki hii, jeshi hilo lilithibitisha kutekeleza mashambulizi mengine ya “kujilinda” kusini mwa Iran Jumatatu, ambapo lilisema lililenga maeneo ya makombora ya Iran pamoja na boti zilizokuwa zikijaribu kutega mabomu katika Mlango wa Hormuz.

    Kutokana na mzozo huo, maelfu ya meli za biashara na mafuta zimekwama katika eneo hilo.

    Centcom imesema mashambulizi hayo yalilenga “kulinda wanajeshi wa Marekani dhidi ya vitisho vya vikosi vya Iran.”

    Iran imeyalaani mashambulizi hayo na kuyataja kuwa “ukiukaji mkubwa wa usitishaji mapigano”, huku ikionya kuwa haitaliacha “tendo lolote la uhasama bila majibu.”

    Rais wa Marekani, Donald Trump, pia ametishia kurejesha mashambulizi makubwa ya mabomu iwapo Iran haitakubali masharti ya Washington.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Uganda yakubali mpango wa Marekani wa kuwaweka Wamarekani karantini kufuatia mlipuko wa Ebola

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Uganda imethibitisha kuwa Marekani imeiomba nchi hiyo kuanzisha kituo maalumu cha kuwaweka karantini na kuwahudumia Wamarekani waliokumbana na virusi vya Ebola, huku hofu ikiongezeka kuhusu kuenea kwa mlipuko huo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

    Akizungumza katika mahojiano na BBC, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Uganda, Diana Atwine, amesema Kampala iko tayari kushirikiana katika mpango huo kutokana na uzoefu mkubwa wa nchi hiyo katika kukabiliana na milipuko ya Ebola.

    “Ndiyo, walitufikia kuhusu kuanzisha kituo cha Ebola hapa. Tuko wazi kwa hilo. Tuna utaalamu mkubwa nchini,” alisema Dkt Atwine.

    Kauli yake imekuja wakati Uganda ikiimarisha udhibiti mipakani baada ya watu wanaoshukiwa kuwa na Ebola kujaribu kuingia nchini humo kutoka maeneo yaliyoathirika zaidi mashariki mwa DRC.

    “Siku tatu zilizopita tuliona wagonjwa wakijaribu kuvuka na kuingia nchini mwetu. Wana ndugu hapa ambao wamekuwa wakiwaambia kuwa wakifika Uganda watapata matibabu na kupona,” amesema.

    Kwa mujibu wa Dkt Atwine, baadhi ya watu hao tayari walikuwa na dalili kali za Ebola na walikiri kupoteza ndugu zao kutokana na ugonjwa huo.

    “Walikuwa wanatoka katika maeneo yaliyo kitovu cha mlipuko, walikuwa na dalili kubwa za Ebola na pia walikuwa wakikiri kuwa wamepoteza baadhi ya ndugu zao.”

    Uganda ina hofu kuwa kuacha mipaka ikiwa wazi kutafanya iwe vigumu kudhibiti maambukizi hayo.

    “Tuligundua kuwa tukiendelea kuweka mipaka wazi hatutaweza kuudhibiti mlipuko huu,” aliongeza.

    Serikali ya Uganda pia imesema inashirikiana na DRC kuanzisha vituo vya upimaji na matibabu karibu na maeneo ya mpakani ili kupunguza watu kuvuka mipaka wakitafuta huduma za afya.

    “Tunafanya kazi pia na DRC kuanzisha vituo vya upimaji na matibabu upande wa mpakani kwa watu wanaotafuta huduma za afya na wanaojaribu kuvuka mpaka.”

    Hatua hizo zinakuja wakati Shirika la Afya Duniani likiendelea kuhimiza juhudi za haraka kudhibiti mlipuko huo wa Ebola ambao umeibua wasiwasi mkubwa wa kiafya katika eneo la Afrika ya Kati na Mashariki.

    Soma zaidi:

  6. Crystal Palace ndio mabingwa wa Kombe la Europa Conference

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Crystal Palace F.C. imeendelea kuandika historia baada ya kutwaa taji lake la tatu ndani ya miezi 12, kufuatia ushindi wa mabao 1-0 dhidi ya Rayo Vallecano katika fainali ya Conference League iliyochezwa mjini Leipzig.

    Mshambuliaji wa Ufaransa, Jean-Philippe Mateta, ndiye aliyefunga bao la ushindi lililowapa Eagles taji lao la kwanza Ulaya na taji la pili kubwa katika historia ya klabu hiyo, baada ya kutwaa kombe la FA msimu uliopita.

    Bao hilo lilipatikana dakika sita baada ya kuanza kwa kipindi cha pili, baada ya kipa wa Rayo Vallecano, Augusto Batalla, kuokoa shuti la Adam Wharton lakini mpira ukamkuta Mateta aliyefunga kwa karibu.

    Mateta sasa amefikisha mabao 16 msimu huu akiwa Palace, licha ya kuwa karibu kuondoka Januari kuelekea AC Milan kabla ya majeraha ya goti kuzuia uhamisho huo.

    Kocha anayeondoka Palace, Oliver Glasner, ameihitimisha safari yake ya miaka miwili na nusu Selhurst Park kwa mafanikio makubwa baada ya kuiongoza timu hiyo kutwaa FA Cup, Community Shield na sasa Conference League.

    Timu zote mbili zilikuwa zikicheza fainali yao ya kwanza kabisa ya mashindano ya Ulaya, jambo lililosababisha mchezo kuanza kwa tahadhari kubwa katika dimba la Red Bull Arena.

    Rayo Vallecano walipata nafasi chache kupitia Alemao na Unai Lopez, lakini Palace walionekana kuwa hatari zaidi kuelekea mapumziko, huku Tyrick Mitchell akikosa nafasi nzuri baada ya pasi safi ya Adam Wharton.

    Katika kipindi cha pili, Yeremy Pino aliipatia Rayo nafasi kadhaa za kusawazisha, ikiwemo mpira wa adhabu uliogonga nyavu za pembeni mara mbili, lakini Palace walibaki imara hadi mwisho na kutwaa ushindi huo wa kihistoria.

  7. Trump asema mazungumzo ya Marekani na Iran bado hayajafikia matokeo yanayoridhisha

    g

    Chanzo cha picha, Getty

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema mazungumzo kati ya Marekani na Iran bado hayajafikia matokeo yanayoridhisha, akionya kuwa huenda Washington ikalazimika “kumalizia kazi” ikiwa makubaliano hayatapatikana.

    Akizungumza Jumatano katika kikao muhimu na wajumbe wa baraza lake la mawaziri, Trump amesema mazungumzo hayo “hayajazaa matunda hadi sasa” na kwamba Marekani “bado haijafurahishwa nayo, lakini itafurahishwa.”

    “Ama iwe kwa njia hii, au tutalazimika kumalizia kazi,” amesema Trump.

    Akirejelea viongozi wa Iran, Trump amesema wanajadili kutoka katika nafasi ya udhaifu.

    “Wanajadili wakiwa katika hali ya udhaifu. Lakini tutaona kitakachotokea. Huenda tukalazimika kurejea na kumalizia kazi, au huenda isiwe hivyo.”

    Trump pia alisisitiza kuwa anaamini viongozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wako tayari kufikia makubaliano.

    Katika kauli nyingine, bila kutoa takwimu rasmi, rais huyo alisema uchumi wa Iran unaendelea kudorora kwa kasi.

    “Uchumi wao unaanguka. Wana mfumuko wa bei wa asilimia 250. Fedha yao haina thamani na mfumo wao mzima wa uchumi unasambaratika,” alisema.

    Katika miezi ya karibuni, Iran imeshuhudia viwango vya juu vya mfumuko wa bei, huku baadhi ya tathmini zikieleza kuwa hali hiyo ni miongoni mwa mibaya zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini humo katika kipindi cha karibu karne moja.

    Trump pia amekanusha uwezekano wa Marekani kulegeza vikwazo dhidi ya Iran ili kuruhusu mafuta ghafi ya Iran kuuzwa katika soko la kimataifa.

    “Hapana, hatuzungumzii kulegeza vikwazo wala kutoa fedha. Hakuna vikwazo vitakavyoondolewa, hakuna fedha zitakazotolewa, hakuna chochote,” amesema.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Hujambo na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya taarifa zinazochipuka za tarehe 28 Mei 2026.