Marekani yaanzisha kituo cha afya Kenya kuwahifadhi Wamarekani waliokumbwa na Ebola

Chanzo cha picha, Getty Images
Japokuwa wizara ya afya ya Kenya ilikanusha kuwa imekubali kuweka karantini ya wamarekani walioambukizwa ebola, Ikulu ya Marekani imethibitisha Jumatano kuwa Marekani inaanzisha kituo cha afya nchini Kenya kitakachopokea Wamarekani waliokumbana na virusi vya Ebola katika maeneo yaliyoathirika na mlipuko unaoendelea.
Kwa mujibu wa afisa wa utawala, Marekani itaanzisha kile alichokiita “kituo cha kisasa kabisa” nchini Kenya kupitia juhudi za pamoja kati ya Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Afya na Huduma za Kibinadamu, na Wizara ya Vita.
Taarifa hiyo iliripotiwa kwanza na gazeti la The Wall Street Journal.
Wakati huohuo, Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio amesema katika kikao cha Baraza la Mawaziri Jumatano kuwa serikali “haitaruhusu mtu yeyote aliyeambukizwa Ebola kuingia Marekani.”
Afisa huyo amesema lengo na muundo wa kituo hicho ni “kutoa huduma bora kwa Wamarekani wanaohitaji kuondolewa haraka” kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ili kuwekwa karantini, akisema hatua hiyo itapunguza “hatari za safari ndefu ya kurejeshwa Marekani.”
“Wagonjwa wa Ebola wanahitaji huduma kwa haraka, na kituo hiki kitawawezesha Wamarekani walioko eneo hilo wanaoambukizwa Ebola kupata huduma za kuokoa maisha haraka iwezekanavyo bila safari ya zaidi ya saa 12 ya ndege ya uokoaji wa kimatibabu,” amesema afisa huyo.
Ameongeza kuwa uwezo wa matibabu katika kituo hicho cha Kenya unatarajiwa kushughulikia “aina zote za ugonjwa wa Ebola, ikiwemo huduma za wagonjwa mahututi,” lakini akaeleza kuwa wagonjwa watatathminiwa mmoja mmoja ili kuamua kama wanahitaji kuhamishwa kwenda vituo vingine vyenye huduma za juu zaidi.
Rubio pia amesisitiza dhamira ya serikali yake ya kudhibiti Ebola, akisema kuwa “kipaumbele cha kwanza cha sera yetu ya mambo ya nje ni kulinda raia wa Marekani.”
“Haturuhusu na hatutaruhusu mtu yoyote aliyeambukizwa Ebola kuingia Marekani,” amesema Rubio, akiongeza kuwa “mashirika mbalimbali ya serikali” yanahusika na “kufuatilia watu ili kuhakikisha hakuna anayeingia nchini akiwa na Ebola na kusababisha tatizo,” akisema hatua hizo zinaendelea vizuri.
Serikali ya Marekani hapo awali ilitumia mamlaka yake chini ya kifungu cha Title 42 kuzuia safari za kuingia Marekani kwa wasio raia, isipokuwa baadhi, waliotembelea DRC, Uganda au Sudan Kusini ndani ya siku 21 zilizopita. Amri hiyo ilipanuliwa wiki iliyopita kujumuisha pia wenye kadi za ukaazi wa kudumu (green card).
Raia wa Marekani waliotembelea nchi hizo wanaelekezwa kupitia viwanja maalum vya ndege kwa uchunguzi wa ziada wa afya, vikiwemo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dulles, John F. Kennedy New York, Hartsfield Jackson Atlanta, na George Bush Intercontinental Houston.





