“Fanyeni hivyo nyumbani pia” – Wanawake wawakosoa mashabiki wa Japan wanaosafisha viwanja vya Kombe la Dunia
Kwa miaka mingi, mashabiki wa soka wa Japan wamekuwa wakisifiwa duniani kwa tabia yao ya kusafisha viwanja baada ya mechi za Kombe la Dunia.
Hata hivyo, safari hii wanakabiliwa na ukosoaji kutoka kwa baadhi ya watu nchini mwao.
Picha zilipoonekana wiki hii zikionesha mashabiki wa Japan wakikusanya taka kwenye majukwaa ya watazamaji baada ya mechi, baadhi ya watu waliona hali hiyo kama kielelezo cha viwango viwili tofauti vya maadili: wanaume wanaosafisha maeneo ya umma lakini wanaacha majukumu ya nyumbani kwa wake zao.
Picha moja iliyosambaa sana mtandaoni ilionesha mwanaume akikusanya taka uwanjani, huku picha nyingine ikimuonesha akiwa amelala kwenye sofa nyumbani akitumia simu yake karibu na kikapu cha nguo chafu, wakati mke wake akiosha vyombo jikoni.
Maandishi yaliyoambatana na picha hiyo yalisema:
"Wanaume nchini Japan wanapaswa kushiriki zaidi kazi za nyumbani," yakiongeza kuwa muda wanaotumia kufanya kazi za nyumbani ni mfupi zaidi duniani.
Chapisho hilo limepata zaidi ya alama 60,000 za kupendwa kwenye mtandao wa X.
Mmoja wa watumiaji wa X alinukuu kauli maarufu ya mwandishi wa Marekani P. J. O'Rourke akisema:
"Kila mtu anataka kuokoa dunia, lakini hakuna anayependa kumsaidia mama kuosha vyombo."
Mtumiaji mwingine aliandika:
"Huenda miongoni mwa watu hawa wanaookota taka kuna mtu aliyeacha mke wake nyumbani akimhudumia mtoto mdogo ili aje kutazama Kombe la Dunia."
Usafi na tabia ya kusafisha baada ya kutumia maeneo ya umma ni sehemu muhimu ya utamaduni wa Japan, na mara nyingi huonekana kama mfano wa nidhamu na uwajibikaji wa kijamii.
Hata hivyo, mjadala huu umeibua maswali kuhusu mgawanyo wa majukumu ya nyumbani na usawa wa kijinsia katika jamii ya Japan.
Unaweza kusoma;