Walowezi wa Kiyahudi wachoma misikiti, magari na mashamba katika Ukingo wa Magharibi
Maafisa wa Palestina wanasema walowezi wa Israel wamechoma moto misikiti miwili, pamoja na magari na mashamba katika eneo la Ukingo wa Magharibi linalokaliwa kwa mabavu, huku mivutano katika eneo hilo ukiendelea kuongeza.
Mashambulizi hayo ya hivi karibuni yanakuja siku mbili baada ya makabiliano kati ya walowezi na Wapalestina karibu na kijiji cha Tal, ambapo Wapalestina wanne na Waisraeli wawili walipoteza maisha.
Pande zote mbili zilituhumiana kwa kuchochea vurugu hizo. Makabiliano hayo yamezidi kuchochea hali ya wasiwasi katika Ukingo wa Magharibi, eneo ambalo limeshuhudia ongezeko la vurugu zinazofanywa na walowezi wenye msimamo mkali dhidi ya Wapalestina, huku wakichochewa na makundi yenye msimamo mkali wa mrengo wa kulia ndani ya serikali ya sasa ya Israel.
Taarifa kutoka upande wa Palestina zinasema kuwa vijiji viwili katika Ukingo wa Magharibi vilishambuliwa na walowezi usiku kucha; magari yaliharibiwa, mali iliibwa na maandishi ya chuki yalipakwa kwenye kuta.
Meya wa Qusra alisema kuwa walowezi walichoma moto msikiti uliokuwa katika hatua za ujenzi.
Abdul Azim Wadi alisema kuwa walowezi walipaka maandishi ukutani mwa msikiti huo, yakiwemo neno "kisasi".
Jeshi la Israel limesema kuwa wanajeshi walitumwa huko Qusra na kwamba polisi watafanya uchunguzi na kukusanya ushahidi.