Ombi la mwanamfalme wa Saudi Arabia kwa Trump alilokataa lilikuwa lipi?

Chanzo cha picha, EPA
Vyanzo vya serikali na wachunguzi walisema Ijumaa kuwa kundi la Ansarullah Houthi, linaloungwa mkono na Iran, limeteka mji muhimu wa pwani na kisiwa katika Mlango-bahari wa Bab al-Mandab nchini Yemen, huku ripoti ya Axios ikieleza kuwa Rais wa Marekani Donald Trump alikataa ombi la mwanamfalme wa Saudi Arabia la kufanya mashambulizi ya anga dhidi ya Wahouthi.
Wahouthi wamefika katika mji wa Dhu Bab nchini Yemen, ulioko moja kwa moja kwenye Mlango bahari wa Bab al-Mandab, na wameteka kisiwa cha Yemen cha Baryim/Miyun kilicho ndani ya mlang bahari huo.
Maeneo yote mawili ni muhimu sana kwa kudhibiti mlango bahari huo, ambao unachukuliwa kuwa mojawapo ya njia muhimu zaidi za usafirishaji wa meli duniani.
Afisa mmoja aliambia mashirika ya habari ya Reuters na AFP kuwa boti zilizobeba wapiganaji wenye silaha wa Houthi zilifika katika Kisiwa cha Baryim/Miyun,ambacho hugawanya mlango bahari huo katika njia mbili za meli, baada ya vikosi vya serikali kuondoka eneo hilo siku ya Alhamisi.
Afisa huyo, aliyeomba kutotajwa jina, aliongeza, "Wahouthi wametwaa udhibiti kamili wa eneo la Bab al-Mandab na Kisiwa cha Miyun kilicho katikati ya mlango bahari huo."
Shahidi mmoja alisema kuwa wanamgambo wa Houthi "wamesambaa kando ya pwani ya Bab al-Mandab, na wanazunguka kwa kutumia magari ya kijeshi."










