Netanyahu amshutumu Meya wa New York kwa 'kuchochea chuki' baada ya tishio la kukamatwa

Netanyahu, amesema anahudhuria Mkutano mjini New York, licha ya meya wa jiji hilo, Zohran Mamdani, hapo awali kutoa tishio la kumkamata.

Muhtasari

Ruka Video uendelee
  • .
  • xx
  • xx
  • xx
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Viongozi wa Uingereza na Ukraine wakutana huku mvutano na Iran ukiongezeka

    Zelensky

    Chanzo cha picha, x/Zelensky

    Waziri Mkuu mpya wa Uingereza, Andy Burnham, amemkaribisha Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, katika kambi ya jeshi la wanamaji ya Uingereza katika mkutano wake wa kwanza na kiongozi wa kigeni tangu aingie madarakani.

    Mkutano huo umefanyika wakati uhusiano wa usalama na kisiasa kati ya Iran, Uingereza na Ukraine ukiendelea kuwa na mvutano. Kwa upande wa Uingereza, ziara hiyo imeelezwa kuwa ishara ya kuendelea kuiunga mkono Ukraine.

    Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alizionya Uingereza na Ukraine kuhusu kile alichosema ni matokeo ya hatua zao dhidi ya Iran.

    Mvutano kati ya Iran na Uingereza umeongezeka baada ya taarifa kwamba ndege ya kivita ya Marekani aina ya B-1 iliondoka katika kituo cha anga cha RAF Fairford nchini Uingereza na kufanya mashambulizi dhidi ya Iran siku moja baada ya Andy Burnham kuapishwa kuwa Waziri Mkuu. Safari ya ndege hiyo ilionekana kupitia mifumo ya kufuatilia ndege.

    Baghaei alisema matumizi ya vituo vya kijeshi vya Uingereza na Marekani, pamoja na kile alichokiita "kukiri" kwa Burnham, ni ushiriki katika kitendo kinachokiuka sheria za kimataifa, na kwamba London inapaswa kuwajibishwa.

    Aliongeza:

    "Tulitarajia serikali mpya ya Uingereza ichukue hatua za busara zaidi kuliko serikali iliyopita, lakini kwa bahati mbaya tumeona imefuata njia ileile, na huenda hata kwa kiwango kikubwa zaidi."

  2. Netanyahu amshutumu Meya wa New York kwa 'kuchochea chuki' baada ya tishio la kukamatwa

    Netanyahu

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amesema anapanga kuhudhuria Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa mjini New York msimu huu wa vuli, licha ya meya wa jiji hilo, Zohran Mamdani, hapo awali kutoa tishio la kumkamata.

    Mamdani baadaye alifuta kauli hiyo, akisema hakuwa na mamlaka ya kisheria ya kumkamata Netanyahu kwa msingi wa hati ya kukamatwa iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), mahakama inayoshughulikia makosa ya kivita.

    Netanyahu, ambaye atakuwa na ziara nyingine tofauti, aliiambia Fox News Jumapili kwamba "hana wasiwasi" kuhusu ahadi ya awali ya Mamdani na akamtuhumu meya huyo kwa kuchochea chuki.

    Netanyahu anatarajiwa kukutana na Rais wa Marekani Donald Trump katika Ikulu ya White House Jumanne na kuhudhuria ibada ya mazishi ya seneta wa zamani Lindsey Graham. Jiji la New York halipo kwenye ratiba ya safari yake hiyo.

    Netanyahu alisema:

    "Anachochea chuki. Anapaswa kuwa meya wa wakazi wote wa New York, Wayahudi, Wakristo, Waislamu, kila mtu."

    Aliongeza kuwa Mamdani anajaribu kugeuza kundi moja la watu dhidi ya jingine, akisema amezungumza na Wamarekani Wayahudi ambao, kwa mujibu wake, wana hofu kwa sasa.

    Netanyahu alirejelea matukio mawili ya kuchomwa visu yaliyotokea New York siku ya Alhamisi, ambapo mshukiwa mmoja alimshambulia mwanaume Myahudi na mwanume mwenye asili ya Asia katika maeneo yaliyokuwa karibu.

    Kwa mujibu wa polisi, mshukiwa huyo anadaiwa kupiga kelele kauli "Allahu akbar" wakati wa mashambulizi hayo. Amefunguliwa mashtaka ya uhalifu wa chuki.

  3. Afrika Kusini yachunguza kifo cha Mnigeria aliyeanguka alipokamatwa na polisi

    Askari wa Afrika Kusini

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mamlaka za Afrika Kusini zinafanya uchunguzi kuhusu kifo cha raia wa Nigeria, Ibeh Chika Simon, mwenye umri wa miaka 42, ambaye alianguka na kufariki alipokuwa akikamatwa na polisi mjini Cape Town wiki iliyopita.

    Kwa mujibu wa matokeo ya awali ya uchunguzi wa maiti, yaliyotolewa na chombo huru kinachosimamia mienendo ya polisi, Simon alikuwa na michubuko na majeraha kadhaa mgongoni na kifuani.

    Mwanadiplomasia wa Nigeria, Ninikanwa Okey-Uche, alisema nchi yake imeshtushwa sana na taarifa za kile alichokiita mbinu za polisi zilizochangia kifo cha Simon.

    Kwa upande wake, polisi wa mkoa wa Western Cape walisema Simon aliugua ghafla na kuanguka alipokuwa akiwekwa chini ya ulinzi baada ya kukamatwa.

    Kifo hicho kinatokea wakati kukiwa na mvutano kati ya Afrika Kusini na Nigeria kutokana na madai kwamba raia wa Nigeria wamekuwa wakilengwa katika mashambulizi ya chuki dhidi ya wageni.

    Mapema mwezi huu, mamlaka za Afrika Kusini pia zilithibitisha kifo cha Mnigeria mwingine mwezi Juni chini ya mazingira yanayofanana.

    Akilaani kifo cha Simon, Okey-Uche, ambaye ni Balozi Mdogo wa Nigeria mjini Johannesburg, alitaka kufanyika kwa uchunguzi wa wazi na wa haki, akidai kuwa kuna mwelekeo unaotia wasiwasi wa vifo visivyoelezwa na madai ya matumizi mabaya ya nguvu dhidi ya raia wa kigeni.

    Alisisitiza kuwa:

    "Washukiwa wana haki ya kufikishwa mahakamani na kufuata mchakato wa sheria; hakuna mamlaka inayopaswa kuwa juu ya sheria."

    Unaweza kusoma;

  4. Jeshi la Israel: Tumenasa droni mbili karibu na mpaka wa Jordan

    Droni

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jeshi la Israel limesema limenasa ndege mbili zisizo na rubani karibu na mpaka wa Jordan, huku likiendelea kuchunguza zilikotokea.

    Katika taarifa yake, jeshi hilo limesema droni hizo hazikuingia ndani ya anga la Israel.

    Takribani siku 10 zilizopita, Israel ilitangaza kuwa ilizuia kombora lililorushwa kuelekea bandari ya Aqaba kwa usaidizi wa vikosi vya Jordan. Bandari hiyo iko umbali wa takribani kilomita tano kutoka bandari ya Eilat nchini Israel.

    Wakati huo, jeshi la Israel lilidai kuwa shambulio hilo lilihusishwa na Iran, na kuonya kuwa mashambulizi hayo yanaweza kusababisha mapigano kuenea hadi ndani ya eneo la Israel.

    Unaweza kusoma;

  5. Trump: Putin na Xi wamenihakikishia hawataiuzia Iran silaha

    Trump

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Donald Trump amesema kuwa viongozi wa Urusi na China, Vladimir Putin na Xi Jinping, wamemuahidi kuwa hawatauza wala kutoa silaha kwa Iran.

    Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa Truth Social, Trump alisema:

    "Rais Xi aliniambia wakati wa mkutano wetu wa hivi karibuni mjini Beijing kwamba hatatoa wala kuuza silaha kwa Iran kwa hali yoyote ile, na hilo linahusu pia kampuni za China."

    Trump aliongeza kuwa Rais wa Urusi, Vladimir Putin, pia alimpa ahadi kama hiyo. Alisema Putin anaelewa kuwa Marekani haiuzi silaha moja kwa moja kwa Ukraine, bali huzipatia nchi za NATO ambazo hulipia gharama, na kwamba hajui silaha hizo hutumika vipi baada ya kuuzwa.

    Trump alihitimisha kwa kusema kuwa:

    "Nchi mbili ambazo mara nyingi hutajwa kuhusiana na Iran, sidhani kama zinahusika. Kama zingekuwa zinahusika, isingekuwa kwa manufaa yao."

    Hata hivyo, shirika la habari la Reuters liliripoti hivi karibuni kwamba mashambulizi ya ndege zisizo na rubani yaliyofanywa na Iran dhidi ya vituo vya CIA katika eneo la Ghuba ya Uajemi yamewafanya wachambuzi wa ujasusi wa Marekani kuchunguza uwezekano wa Urusi kuisaidia Iran kwa taarifa za kijasusi.

    Ripoti hiyo ilinukuu vyanzo vinne vinavyofahamu shughuli za ujasusi wa Marekani, ingawa majina yao hayakuwekwa wazi.

    Kwa mujibu wa Reuters, maafisa wa ujasusi wa Marekani bado hawajafikia hitimisho la mwisho kuhusu iwapo Urusi ilihusika. Hata hivyo, wanaamini uwezekano huo upo kutokana na ushirikiano wa kiufundi kati ya Urusi na Iran, pamoja na usahihi na ufanisi wa mashambulizi hayo.

    Taarifa za awali kuhusu Urusi kuisaidia Iran kulenga maslahi ya Marekani zilikuwa zimewahi kuripotiwa na vyombo vya habari na kuthibitishwa na baadhi ya maafisa wa Marekani. Lakini uchunguzi huu mpya unaohusu uwezekano wa Urusi kusaidia Iran kulenga vituo vya CIA haukuwa umewekwa wazi hapo awali.

    Kwa mujibu wa Reuters na vyombo vingine vya habari, takribani vituo viwili vya CIA vililengwa mwezi Machi mwaka huu:

    • Makao ya CIA ndani ya Ubalozi wa Marekani mjini Riyadh, Saudi Arabia.
    • Kituo kingine mashariki mwa Iraq.

    Baadhi ya vyanzo vya Reuters vilisema kuwa vituo vingine vya CIA pia vililengwa, lakini havikutoa maelezo zaidi.

    Unaweza kusoma;

  6. Iran: Hatuna mazungumzo na Marekani kwa sasa, tutaendelea kujibu mashambulizi

    silaha

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, amesema kuwa kwa sasa hakuna mazungumzo yoyote yanayoendelea kati ya Iran na Marekani.

    Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, Baghaei alizitaja taarifa zinazodai kuwa Iran imeomba mazungumzo na Marekani kuwa ni "uzushi wa kutengeneza habari."

    Alisema kuwa wakati Marekani inaendelea na kile alichokiita vitendo vya uchokozi na mashambulizi dhidi ya Iran, kipaumbele cha Tehran ni kujilinda. Hata hivyo, alibainisha kuwa wapatanishi wanaweza kuwasilisha ujumbe kutoka upande wa Marekani kuhusu hali ya sasa ya eneo hilo.

    Kuhusu kusitishwa kwa mashambulizi ya Marekani, Baghaei alisema:

    "Iran haitairuhusu Marekani kuamua wakati wa vita na wakati wa amani."

    Aidha, alisisitiza kuwa hali ya sasa haiwezi kuelezewa kama usitishaji wa mapigano .

    Kwa mujibu wa Baghaei, hali imekuwa tulivu zaidi katika siku za hivi karibuni kutokana na mkakati wa vikosi vya jeshi la Iran, akionya kuwa hatua yoyote mpya kutoka Marekani itakabiliwa na jibu kali kutoka Iran.

    Katika mkutano huo, Baghaei pia alisema kuwa Mlango wa Bahari wa Hormuz bado umefungwa.

    Akizungumzia shambulio la Ukraine dhidi ya meli katika Bahari ya Caspian, alidai kuwa tukio hilo linakumbusha vitendo vya wanaharakati wenye misimamo mikali kabla ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia.

    Aliitaja hatua ya Ukraine kuwa haramu na isiyo na msingi, akisisitiza kuwa haitaachwa bila majibu.

  7. Meli yenye bendera ya Tanzania yakamatwa na maharamia Somalia

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Meli ya wafanyabiashara yenye bendera ya Tanzania imekamatwa na maharamaia wa Somalia katika Ghuba ya Aden.

    Meli hiyo kwa jina MT Asana ina mafuta na kemikali na ilikuwa na wafanyakazi 20, wanane kutoka Ujerumani na 10 kutoka Ufilipino.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Ujerumani ilisema kama kanuni yake, haitoi maoni kuhusu matukio ya raia wa Ujerumani kutekwa nyara nje ya nchi.

    Shirika la United Kingdom Maritime Trade Operations (UKMTO) lilisema wiki iliyopita kuwa meli iliyovamiwa na watu wasioidhinishwa katika Ghuba ya Aden ilikuwa imeelekezwa kuingia katika maji ya Somalia, na tukio hilo lilitambuliwa rasmi kama utekaji wa meli.

    Maharamia wa Somalia walisababisha machafuko makubwa katika maji yaliyoko kando ya pwani ya nchi hiyo katika Pembe ya Afrika kati ya mwaka 2008 na 2018.

    Baada ya kipindi cha utulivu, shughuli za uharamia zilianza kuongezeka tena mwishoni mwa mwaka 2023.

  8. Nyota mchezaji wa zamani wa Marekani arejeshwa Kenya

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mchezaji wa zamani wa raga wa Kenya na beki wa zamani wa ligi ya mpira wa miguu ya Marekani (NFL), Daniel Adongo, amerejeshwa nchini Kenya na Idara ya Uhamiaji na Utekelezaji wa Forodha ya Marekani (ICE) baada ya mamlaka za uhamiaji za Marekani kusema kuwa alizidisha muda wa kukaa nchini humo baada ya visa yake kuisha.

    Adongo ambaye pia aliweka historia alipohamia kwenye soka la Marekani na kuchezea Indianapolis Colts.

    Kwa mujibu wa ICE na taarifa za vyombo vya habari vya Marekani, Adongo, mwenye umri wa miaka 37, alifurushwa Marekani tarehe 20 Juni baada ya jaji wa uhamiaji kutoa amri ya kuondolewa nchini humo mnamo mwezi Machi.

    Mamlaka zilisema uamuzi huo ulitokana na kubainika kuwa alikuwa ameendelea kubaki nchini Marekani baada ya muda wa visa yake kuisha mwaka 2016.

    ICE ilisema kuondolewa kwa Adongo pia kulitokana na rekodi yake ya makosa ya uhalifu nchini Marekani, ikiwemo hukumu ya mwaka 2020 kwa kosa la uhalifu.

    Idara hiyo ilisema Adongo alikuwa amewahi kukamatwa awali kwa tuhuma zilizojumuisha vitisho vya uhalifu, shambulio na tabia ya kuvuruga amani.

    Hata hivyo, ICE haikuonyesha katika taarifa yake ikiwa visa hivyo vilipelekea kupatikana kwa hukumu nyingine za hatia.

  9. Bei ya mafuta yashuka huku Iran na Marekani zikisitisha mashambulizi

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Bei za mafuta zimeshuka baada ya Marekani kusitisha kwa muda mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Iran.

    Mafuta ghafi yameshuka kwa takriban asilimia tano.

    Mashambulizi ya mwisho yalifanyika usiku wa Alhamisi.

    Iran inasema nayo imesitisha mashambulizi katika eneo hilo huku mazungumzo kupitia wapatanishi kutoka Oman yakipiga hatua.

    Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, alisema Rais Trump alitaka kuyapa mazungumzo ya kidiplomasia muda zaidi.

    Ripoti za vyombo vya habari vya Marekani zinaeleza kuwa wasiwasi kuhusu kupungua kwa akiba ya makombora ya kuzuia mashambulizi huenda pia ulichangia uamuzi wa kusitisha mashambulizi hayo.

    Soma zaidi:

  10. Rais wa Syria atafuta makubaliano ya usalama na Israel

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Syria Ahmed al-Sharaa amesema anajitahidi kufikia makubaliano ya kiusalama na Israel.

    Al-Sharaa alisema makubaliano hayo yanaweza kutoa mwelekeo wa amani ya kina kati ya nchi hizo mbili bila kuathiri haki ya Syria kuhusu Milima ya Golan, eneo ambalo Israel ililiteka kutoka Syria katika vita vya siku sita vya mwaka 1967 na kulinyakua rasmi mwaka 1981.

    Sharaa aliongeza kuwa Syria ilikuwa ikijaribu kushirikisha kundi kubwa la nchi ili kuishinikiza Israel kufuata sera yenye uwiano zaidi kuelekea Syria.

    "Tunaepuka kuingia katika makabiliano," aliongeza.

    Muda mfupi baada ya Rais wa zamani wa Syria, Bashar Al Assad, kuondolewa madarakani na vikosi vya waasi vilivyokuwa vikiongozwa na Sharaa mnamo mwezi Desemba 2024, wanajeshi wa Israel waliingia nchini Syria na kuteka maeneo ya kimkakati.

    Wanajeshi wa Israel waliingia katika eneo lisilo la kijeshi ndani ya Syria, ikiwa ni pamoja na upande wa Syria wa Mlima Hermon, ambao unaangalia mji mkuu wa Damascus.

    Tangu wakati huo, jeshi la Israel limefanya mashambulizi nchini Syria na kuwakamata baadhi ya watu kutoka ndani ya nchi hiyo.

    Israel pia imeingilia kati katika kile inachokiita operesheni za kulinda jamii ya wachache wa Druze wanaoishi kusini-magharibi mwa Syria.

    Soma zaidi:

  11. Uganda ni miongoni mwa vikosi vya usalama vitakavyoingia Gaza

    .

    Uganda kuwa miongoni mwa kikosi cha kimataifa cha kulinda amani kuingia Ukanda wa Gaza.

    Tayari Uganda imetoa idhini ya awali kufuatia ombi la moja kwa moja kutoka kwa Rais wa Marekani, Donald Trump hadi kwa Rais Yoweri Museveni.

    Inasemekana Rais Trump aliiomba Uganda kuunga mkono kuanzishwa kwa kikosi cha kimataifa nchini Gaza kitakacholenga kukomesha machafuko, kulinda raia, na kuharakisha utoaji wa misaada ya kibinadamu pamoja na juhudi za ujenzi upya.

    Afisa wa Israel alisema baraza la mawaziri la usalama la Netanyahu lilipitisha mfumo wa kisheria utakaoruhusu kikosi hicho kuingia Gaza huku Netanyahu akitarajiwa kuondoka kuelekea Washington siku ya Jumatatu na kukutana na Rais Trump siku ya Jumanne.

    Afisa huyo alisema hicho kitakuwa Kikosi cha Kimataifa cha Uimarishaji wa Usalama (International Stabilization Force), kitakachohusisha wanachama 200 kutoka nchi "rafiki" ambazo ni pamoja na Morocco, watakaopelekwa katika maeneo ambayo hayako chini ya udhibiti wa Israel. Nchi husika zitahitajika kupata idhini ya Israel kabla ya kuruhusiwa kuingia Gaza.

    Sehemu kubwa ya Ukanda wa Gaza bado imeharibika vibaya kutokana na miaka miwili ya vita vilivyochochewa na mashambulizi yaliyoongozwa na Hamas dhidi ya Israel mnamo Oktoba 7, 2023.

    Baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano kufikiwa mnamo mwezi Oktoba, Rais wa Marekani Donald Trump aliwasilisha mpango wa amani kwa Gaza uliopendekeza kuongezwa kwa misaada ya kibinadamu, kuundwa kwa utawala wa kiraia unaoongozwa na wataalamu wa Kipalestina, Hamas kuweka silaha chini, na vikosi vya Israel kujiondoa Gaza.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Watu watatu wauawa na wanne kujeruhiwa katika katika tamasha la chakula Marekani

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Watu watatu wameuawa na wengine wanne kujeruhiwa baada ya shambulio la risasi lililotokea katika tamasha la chakula karibu na Space Needle mjini Seattle, Marekani.

    Mkuu Msaidizi wa Polisi wa Seattle, Tyrone Davis, amesema watu watatu wamefariki dunia kutokana na tukio hilo.

    Kwa mujibu wa Davis, waathiriwa wawili walifariki dunia papo hapo eneo la tukio kutokana na majeraha mabaya waliopata, huku mwathiriwa wa tatu aliyekimbizwa katika Hospitali ya Harborview Medical Center naye akifariki dunia baadaye kutokana na majeraha aliyoyapata.

  13. Waziri wa Somalia azuiwa kuingia Kenya

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri wa masuala ya nchi katika Ofisi ya Rais, Abshir Bukhaari, ameripotiwa kuzuiwa kuingia nchini Kenya na baadaye kurejeshwa Mogadishu, kwa mujibu wa taarifa kutoka vyanzo mbalimbali.

    Maafisa wa uhamiaji wa Kenya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) jijini Nairobi wanadaiwa kumzuia kuingia nchini siku ya Jumapili kutokana na pasipoti ya Kenya aliyokuwa akisafiria.

    Serikali za Somalia na Kenya hazikuwa zimetoa kauli rasmi kuhusu tukio hilo.

    Taarifa hiyo inafuatia tukio jingine lililotokea takribani mwezi mmoja uliopita (Juni 24), lililomhusisha Naibu Waziri Mkuu wa Somalia, Jibril Abdirashid Haji, ambaye pia aliripotiwa kunyimwa kuingia nchini Kenya na kurejeshwa Somalia kutokana na madai kuwa alikuwa na pasipoti ya Kenya iliyopatikana kwa njia ya udanganyifu.

    Naibu Waziri Mkuu huyo aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa JKIA kwa ndege ya Shirika la Saacid Airlines kutoka Mogadishu na kuwasilisha pasipoti halali ya kidiplomasia ya Somalia pamoja na visa ya kuingia Kenya.

    Taarifa zinasema maafisa wa uhamiaji walimtilia shaka baada ya kushukiwa kuwa pia alikuwa na pasipoti ya Kenya iliyopatikana kwa njia isiyo halali.

    Vyanzo vinavyofahamu suala hilo viliviambia vyombo vya habari vya ndani kuwa afisa huyo wa Somalia alikiri kuwa na pasipoti ya Kenya, lakini alikataa kuikabidhi, akisema suala hilo linapaswa kushughulikiwa kupitia mchakato wa mahakama.

    Mvutano huo ulisababisha Haji kupelekwa katika eneo la mapumziko la wageni maalumu la uwanja wa ndege wakati uchunguzi ukiendelea, kabla ya baadaye kusindikizwa kupanda ndege ya Shirika la Daallo Airlines iliyokuwa ikielekea Mogadishu, na hivyo kunyimwa rasmi ruhusa ya kuingia nchini Kenya.

    Hadi wakati huo, serikali za Kenya na Somalia hazikuwa zimetoa taarifa rasmi kuhusu tukio hilo.

  14. Wafcon 2026: Wawakilishi wa Afrika Mashariki Kenya wachapwa na Morocco

    .

    Chanzo cha picha, Backpage Pix

    Michezo ya kandanda ya mataifa ya Afrika kwa wanawake zimeanza kutimua vumbi jana Jumapili nchini Morocco na kuchezwa michezo miwili ya kukata utepe.

    Katika mchezo wa kwanza Algeria waliwanyuka Senegal 2-0 magoli ya dakika ya 42 na 85 huku wenyeji Morocco wakiwanyanyasa wawakilishi wa Afrika Mashariki Kenya kwa ushindi wa magoli 4-0.

    Magoli matatu yalitiwa kimiani ndani ya dakika 32 za kwanza la nne likafungwa dakika 2 tu baada ya mapunziko.

    Leo kuna michezo miwili. Afrika Kusini itakipiga na wawakilishi wengine wa Afrika Mashariki Tanzania saa mbili usiku kabla ya Ivory Coast kutoana jasho na majirani zao wa Kaskazini, Burkina Faso.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Macron aitisha kikao cha dharura huku moto mkubwa wa nyika ukiendelea

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ataongoza kikao cha dharura cha baraza la mawaziri leo Jumatatu huku moto wa nyika ukikaribia mji wa Bordeaux, ulioko kusini-magharibi mwa nchi hiyo.

    Wimbi jingine la joto linatarajiwa kufanya juhudi za kudhibiti moto huo unaoendelea kuenea kuwa vigumu. Moto huo kwa sasa uko umbali wa takribani kilomita 15 (maili 9) kutoka Bordeaux, meya wa mji huo, Thomas Cazenave, alisema. Awali, alisema hakuna mpango wa kuwahamisha wakazi wapatao 850,000 wa mji huo.

    Ufaransa imekuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika zaidi, huku hekta 42,000 zikiathirika na moto kusini-magharibi mwa nchi hiyo. Hilo limeufanya kuwa miongoni mwa moto mkubwa zaidi wa misitu nchini humo tangu Vita vya Pili vya Dunia.

    Kwa jumla, zaidi ya watu wapatao laki mbili na ishirini wamehamishwa katika eneo la kusini-magharibi mwa Ufaransa.

    Kapteni Nicolas Braz, mmoja wa viongozi wa operesheni ya kuzima moto, amesema moto huo ulikuwa na upepo mkali sana ukiambatana na vimbunga vidogo”, na kuongeza kuwa ulikuwa “haueleweki na usioweza kudhibitiwa.

    Wakazi wa Le Porge, mojawapo ya miji ya pwani iliyoathiriwa na moto huo, wameanzisha mtandao wa kujitolea wa kusaidia wazima moto waliochoka. Wanawapikia chakula na kuwapa mahali pa kupumzika kati ya zamu zao.

    Zaidi ya nyumba 150 zimeharibiwa katika mji huo wenye wakazi 3,500.

    Wakaazi wengi wanasema wamehuzunishwa na tukio hilo ulioathiri misitu yake, wanyamapori na watu waliopoteza vitu vingi,” alisema Augonnet.

    “Kwa sasa, tunazingatia kuchukua hatua, hivyo hatuna muda wa kufikiria sana. Nadhani sehemu yenye changamoto itakuja baadaye, wakati wa kuanza tena ujenzi.

    Wakati huo huo nchini Uhispania, moto unaendelea kusambaa, huku zaidi ya watu 90,000 wakihamishwa kutoka maeneo yanayozunguka Madrid na Ávila.

    Takriban hekta 77,000 zimeathiriwa na moto nchini Uhispania, alisema Waziri wa muda wa Ikolojia, Sara Aagesen, siku ya Jumapili.

    Soma Zaidi:

  16. Iran: Tutasitisha mashambulizi iwapo Marekani haitatushambulia tena

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Iran ameliambia shirika la habari la Reuters siku ya Jumapili kuwa itasitisha mashambulizi yake, mradi tu Marekani nayo iendelee kusitisha mashambulizi yake, kulingana na afisa mmoja mwandamiz.

    Hatua hiyo imekuja baada ya Marekani kusitisha kwa muda kampeni yake ya mashambulizi ya anga, kufuatia washauri wa Rais Donald Trump kumweleza kuwa walikuwa wakikabiliwa na wasiwasi kuhusu kupungua kwa akiba ya silaha za Marekani.

    Baada ya usiku 13 mfululizo wa mashambulizi makali ya anga ya Marekani dhidi ya Iran, Wizara ya Ulinzi ya Marekani ilisisitisha operesheni hiyo mwishoni mwa Ijumaa.

    Hakukuwa na mashambulizi yoyote ya Marekani yaliyoripotiwa Jumamosi wala Jumapili.

    Kwa upande wake, Iran, ambayo ilikuwa ikijibu kila usiku wa mashambulizi ya Marekani kwa kushambulia nchi jirani zinazohifadhi kambi za kijeshi za Marekani, pia haijafanya mashambulizi yoyote kwa siku mbili zilizopita hadi sasa.

    Afisa huyo wa Iran, ambaye alizungumza na shirika la habari la Reuters kwa sharti la kutotajwa jina, alisema msimamo wa Tehran unaendelea kuwa "shambulio kwa shambulio." Alieleza kuwa, "Iwapo mashambulizi yatasitishwa, Iran pia itasitisha operesheni zake. Ujumbe huo tayari umefikishwa kwa Marekani."

    Kwa upande mwingine, Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, aliviambia kipindi cha Fox News Sunday pamoja na vyombo vingine vya habari vya Marekani kuwa Rais Donald Trump aliamua kusitisha kwa muda mashambulizi ya Marekani ili kutoa nafasi zaidi kwa juhudi za kidiplomasia.

    Akizungumza kuhusu uamuzi wa Rais Donald Trump, Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, alisema:

    "Antoa fursa kwa mazungumzo yaendelee; anatoa muda kidogo ili yaweze kusonga mbele."

    Maafisa wa jeshi la Marekani katika siku za karibuni wameonya kuwa mashambulizi ya mabomu yaliyofanywa katika kipindi cha wiki mbili zilizopita, yaliyolenga kuzuia vitisho vya Iran dhidi ya usafirishaji wa meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz—njia ya maji ambayo imesababisha mvutano katika vita hivyo—yalikuwa yamekaribia kumaliza maeneo lengwa yaliyokuwa yamechaguliwa mapema kwa ajili ya kushambuliwa, kwa mujibu wa afisa mmoja wa Marekani aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina.

    Soma Zaidi:

  17. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara, tarehe ni 27/07/2026