Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon ni mashambulizi makali zaidi tangu usitishaji vita ulipoanza
Makumi ya watu waliuawa katika wimbi kali la mashambulizi ya anga ya Israeli kusini na mashariki mwa Lebanon siku ya Jumanne, baada ya Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu, kuapa kuongeza kasi ya hatua za kijeshi dhidi ya Hezbollah.
Wizara ya Afya ya Lebanon ilisema kuwa takribani watu 31 waliuawa katika mashambulizi hayo ya hivi karibuni, wakiwemo watoto kadhaa.
Jeshi la Israel lilisema lililenga zaidi ya maeneo 100 ya miundombinu ya Hezbollah pamoja na wapiganaji wa Hezbollah, katika mojawapo ya usiku wenye mashambulizi makubwa zaidi tangu usitishaji vita uliosimamiwa na Marekani uanze katikati ya Aprili.
Haya yalitokea baada ya Netanyahu kusema wiki hii kwamba alikuwa amewaagiza maafisa wake "kukanyaga mafuta zaidi" katika operesheni za kuilenga Hezbollah.
Mapema Jumatano asubuhi, ving'ora vya tahadhari vilisikika kaskazini mwa Israeli baada ya kombora kurushwa kutoka Lebanon kuelekea Israeli, kulingana na taarifa kutoka jeshi la Israeli.
Jeshi hilo liliongeza kuwa kombora hilo lilitua katika eneo la wazi, na hakukuwa na taarifa za majeruhi.
Wakati wa mkutano wa baraza la usalama siku ya Jumanne, Benjamin Netanyahu alisema kuwa Israeli ilikuwa "ikiendeleza operesheni yake nchini Lebanon kwa kina zaidi."
Alisema: "Jeshi la Israeli linafanya operesheni kwa kutumia vikosi vikubwa ardhini na linadhibiti maeneo ya kimkakati," akiongeza kuwa linafanya kazi ya "kuimarisha ukanda wa usalama" ili kulinda wakazi wa kaskazini mwa Israeli dhidi ya mashambulizi ya Hezbollah.
Usitishaji vita huo umeendelea kukiukwa mara kwa mara na pande zote mbili, jambo linalotishia kuvuruga mazungumzo magumu yanayoendelea ya kumaliza vita kati ya Marekani, Israel na Iran.
Mashambulizi ya anga ya Israeli pamoja na mashambulizi ya mizinga yaliendelea kila siku, hasa kusini mwa Lebanon, huku Hezbollah ikiendelea kurusha makombora na ndege zisizo na rubani kuelekea miji ya kaskazini mwa Israeli na dhidi ya vikosi vya Israeli vinavyokalia sehemu za kusini mwa Lebanon.
Vyombo vya habari vya ndani viliripoti kuwa mashambulizi ya anga yalilenga mji wa Mashghara katika Bonde la Bekaa na Burj al-Shamali kusini mwa Lebanon.
Vyombo vya habari vya serikali viliripoti kuwa baadhi ya mashambulizi hayo yalifanyika karibu na Beaufort Castle, ngome yenye takribani miaka 900, ambayo UNESCO inaielezea kama "moja ya mifano iliyohifadhiwa vizuri zaidi ya majumba ya enzi za kati" katika eneo hilo.
Katika taarifa ya video iliyotolewa Jumatatu, Benjamin Netanyahu alisema kuwa Israeli itaongeza idadi na ukubwa wa mashambulizi yake dhidi ya Hezbollah kujibu mashambulizi ya kundi hilo linaloungwa mkono na Iran, ikiwemo mashambulizi kwa kutumia ndege zisizo na rubani za nyuzi za optic ambazo zinaweza kukwepa mifumo ya ulinzi ya Israeli.
Aliapa kusema: "Tutawapa pigo kubwa la kuwaangamiza."
Tangazo hilo lilisababisha taharuki katika vitongoji vya kusini mwa Beirut, ngome ya Hezbollah, huku wakazi wakionekana wakikimbia eneo hilo baada ya matamshi ya Netanyahu. Maelfu ya magari yalijaa barabarani huku familia zikijaribu kukimbilia maeneo salama.
Ingawa mashambulizi hayo hayakufika mji mkuu, ndege za kivita za Israeli zilianzisha mawimbi ya mashambulizi kote Lebanon katika kipindi chote cha jioni hadi alfajiri ya Jumanne. BBC ilihesabu mashambulizi kadhaa katika takriban maeneo 50.
Usiku wa kuamkia Jumatano, ndege za kivita za Israeli zilivamia na kulipua mji wa Shaqra, zikafanya operesheni kubwa ya upekuzi katika mji wa Khiam, na pia kushambulia mji wa Frun, kulingana na Shirika la Habari la Taifa la Lebanon.
Mwanaume mmoja na mke wake waliuawa katika shambulizi la anga lililolenga nyumba yao katika mji wa Arab Salim kusini mwa Lebanon Jumatatu jioni, huku watu wengine wawili wakiuawa katika mji wa Kawthariyat al-Ruz, kwa mujibu wa Shirika la Habari la Taifa.
Wakati wa usiku, nyumba kadhaa katika mji wa Mashghara ziliharibiwa na mashambulizi ya anga ya Israeli.
Wizara ya Afya ya Lebanon ilisema kuwa miili ya watu 11, akiwemo mwanamke mmoja na watoto wawili, ilitolewa kutoka kwenye vifusi. Iliongeza kuwa watu wengine 15 walijeruhiwa.
Miongoni mwa waliojeruhiwa alikuwa mvulana mdogo aitwaye Mohammed. Video zinaonesha timu za uokoaji zikifanya kazi usiku kucha katikati ya vifusi kabla ya kufanikiwa kumtoa akiwa hai. Mohammed ana umri wa miaka saba.
"Nilipoamka, nilihisi siwezi kusogea, na nilikuwa nimezungukwa na giza," Mohammed aliiambia BBC akiwa amelala kitandani hospitalini huku akizungukwa na wanafamilia wake.
Aliongeza: "Nilisikia sauti za wanaume waliokuwa wakiniokoa. Iliwachukua muda mrefu kunitoa."
Kichwa chake kilikuwa kimefungwa bandeji, huku mikwaruzo na majeraha yakionekana mikononi na miguuni mwake.
Mohammed alikuwa amelala kitandani mwake wakati kombora lilipoipiga nyumba yao, na kumuua baba yake pamoja na dada zake wawili.
Mashghara inaonekana kama mji uliotelekezwa. Magari machache yalikuwa yakipita karibu nasi ili kukagua vitambulisho vyetu, lakini hakukuwa na dalili za maisha ya kawaida.
Ahmed, alitupeleka katika maeneo yaliyokuwa yamepigwa na baadhi ya mashambulizi ya usiku. Mandhari yalikuwa ya kutisha, huku nyumba na maduka yakiwa yameharibiwa.
Ahmed alisema: "Mimi si mwanachama wa Hezbollah, lakini watu wote wa mji huu wanaunga mkono upinzani, na adui [Israeli] hamwachi mtu yeyote."
Kisha sauti ya ndege ilikatiza mazungumzo yake. Mlipuko mkubwa ulitikisa eneo hilo, na tulilazimika kuondoka.
Baadaye, video zilizowekwa kwenye mitandao ya kijamii zilionesha mlipuko mkubwa barabarani karibu na eneo tulilokuwa tukirekodia.
Jeshi la Israeli lilitoa picha za angani kutoka Mashghara, ambazo lilisema zinaonesha mashambulizi kadhaa dhidi ya "maeneo ya miundombinu ya Hezbollah ambapo shughuli za kigaidi ziligunduliwa." Liliongeza kusema: "Wakati wa shambulizi hilo, magaidi waliangamizwa."
Jeshi la Israeli pia lilisema kuwa usiku kucha lililenga zaidi ya maghala 90 ya silaha, vituo vya amri, maeneo ya uangalizi na miundombinu mingine inayotumiwa na Hezbollah kusini mwa Lebanon.
Jumanne asubuhi, jeshi hilo lilitoa amri mpya za kuhama katika baadhi ya maeneo ya Lebanon, likiishutumu Hezbollah kwa kukiuka masharti ya usitishaji vita kati ya serikali za Israel na Lebanon, ambao ulianza kutekelezwa Aprili 17.
Msemaji wa jeshi, Kanali Avichay Adraee, alisema kwa Kiarabu kuwa ukiukaji wa mara kwa mara uliofanywa na Hezbollah uliwaacha wanajeshi wa Israeli bila chaguo jingine isipokuwa kuchukua hatua.
Hezbollah ilisema kuwa ililenga kambi tatu za kijeshi na eneo moja la kijeshi kaskazini mwa Israeli "kujibu ukiukaji wa usitishaji vita uliofanywa na Israeli."
Amri ya Benjamin Netanyahu ya kuongeza mashambulizi ya Israeli ilikuja baada ya jeshi kusema kuwa mwanajeshi mmoja aliuawa katika mapigano kusini mwa Lebanon siku ya Jumapili, jambo lililofikisha idadi ya wanajeshi wa Israeli waliouawa huko kutokana na mashambulizi ya Hezbollah tangu mzozo huo uanze Machi 2 hadi 23, pamoja na mkandarasi mmoja raia.
Wizara ya Afya ya Lebanon inasema kuwa mashambulizi ya Israeli katika kipindi hicho hicho yalisababisha vifo vya takribani watu 3,185.