Kesi ya uhaini ya Tundu Lissu yaendelea baada ya kusimama kwa miezi 5
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, amefikishwa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam leo, Agosti 10, 2026, kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa kwa kesi ya uhaini inayomkabili.
Kesi hiyo imeanza tena baada ya kusimama kwa takribani miezi mitano tangu Februari 24, 2026.
Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini chini ya Kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, linalohusishwa na kauli alizotoa kuhusu kusudio la kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kesi hiyo inasikilizwa kwa mfululizo kuanzia leo hadi Septemba 7, 2026, chini ya Jopo la Majaji watatu, likiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru.
Vikao vya maandalizi ya uendeshaji wa kesi hiyo vilifanyika kuanzia Agosti 5, 2026, vikihusisha Mahakama, upande wa Jamhuri, mshitakiwa Tundu Lissu pamoja na mawakili wake.
Kwa sasa, kesi hiyo ipo katika hatua ya usikilizwaji wa ushahidi.
Baadhi ya mashahidi, wakiwemo askari polisi na mashahidi wasiokuwa askari ambao ni mashahidi wanaolindwa, tayari wametoa ushahidi wao.
Lissu amekuwa akishikiliwa gerezani tangu alipokamatwa Aprili 9, 2025, na kushtakiwa siku iliyofuata kwa makosa ya uhaini na uchochezi.