M23 yapinga hatua ya kusitishwa kwa masomo katika vyuo vikuu vya Goma na Bukavu
Kundi la waasi la M23 limekosoa uamuzi wa hivi karibuni wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), wa kusimamisha kwa muda masomo katika vyuo vikuu kadhaa, katika miji ya Goma na Bukavu, kutokana na sababu za kiusalama.
Katika taarifa iliyotolewa na kundi hilo, imesema kuwa uamuzi uliochukuliwa na mamlaka za Kinshasa “ulikuwa wa haraka na haukuzingatia madhara yanayoweza kujitokeza”
M23 inasema kuwa kulingana na katiba ya taifa hilo, kila mtu ana haki ya kupata elimu, na elimu haifai kutumiwa katika maslahi ya kisiasa.
“Hakuna mwanafunzi anayepaswa kulazimishwa kupoteza mwaka wa masomo au elimu yake kutokana na hali ambayo nchi inakabiliwa nayo,” taarifa ya M23 imesema.
Mwaka uliopita, M23 iliteka maeneo kadhaa yaliyokuwa chini ya udhibiti wa majeshi ya serikali ya DRC ikiwemo mji wa Goma na Bukavu.
Ingawa M23 inasema maeneo inayodhibiti yako salama, mapigano ya hapa na pale kati ya kundi hilo na majeshi ya serikali yamekuwa yakishuhudiwa.
Waziri wa Elimu ya Juu na Vyuo Vikuu nchini DRC, Prof Marie-Thérèse Sombo Ayanne, amesema ukosefu wa usalama umetatiza shughuli za kawaida za taasisi za elimu.
Waziri huyo amewaagiza viongozi wa vyuo vilivyoko katika maeneo salama kuwapokea wanafunzi kutoka maeneo yaliyoathiriwa na vita ili waweze kuendelea na masomo yao.
Soma pia: