Ukatili unaweza kutokea hivi karibuni katika jiji la El Obeid, Sudan

Chanzo cha picha, Getty Images
Muungano wa zaidi ya nchi 20 umeonya kuhusu hatari inayoweza kutokea ya ukatili mkubwa nchini Sudan, ukisema kuwa hadi raia 500,000 wanaweza kuwa katika hatari huku vurugu zikiongezeka karibu na mji wa El Obeid katika eneo la North Kordofan.
Muungano wa Kuzuia Ukatili na Kuendeleza Haki nchini Sudan ulisema kuwa takriban raia 50 wameuawa katika kipindi cha siku kumi mfululizo za mashambulizi ya ndege zisizo na rubani katika El Obeid na kaskazini mwa Kordofan.
Pia ulitaja “taarifa za kuaminika za vurugu zinazolenga makundi ya kikabila ikiwemo unyanyasaji wa kingono na wa kijinsia,” na kuonya kuwa zaidi ya watu 100,000 waliokimbia makazi yao ndani ya nchi wanaweza kuwa hatarini ikiwa mapigano yataongezeka.
"Tunatoa wito kwa Vikosi vya Rapid Support Forces (RSF) kusitisha mara moja mashambulizi yao dhidi ya El Obeid," muungano huo ulisema, huku ukiwataka wahusika wote kupunguza mivutano na kuzingatia sheria za kimataifa za kibinadamu.
Pia ulitoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuongeza shinikizo kwa pande zote zinazopigana ili kuzuia ukatili zaidi.
Onyo hilo linakuja wakati Umoja wa Mataifa pia umeonyesha wasiwasi kuhusu taarifa za uwezekano wa mashambulizi ya ardhini dhidi ya mji huo, ambao ni mojawapo ya vituo muhimu zaidi vya misaada ya kibinadamu na biashara nchini Sudan.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, na Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu, Volker Türk, wote wameelezea wasiwasi wao kuhusu hali inayoendelea kuzorota.
"Katibu Mkuu ameshtushwa na taarifa za uwezekano wa mashambulizi ya ardhini yanayoweza kutokea muda wowote huko El Obeid," msemaji wa Umoja wa Mataifa, Stéphane Dujarric, alisema katika taarifa.
El Obeid ipo kwenye njia muhimu inayounganisha maeneo yanayodhibitiwa na RSF huko Darfur na maeneo yanayodhibitiwa na jeshi mashariki mwa Sudan. Mji huo pia ni kitovu muhimu cha usafirishaji wa misaada ya kibinadamu katika eneo lote la Kordofan. Aidha, inahifadhi idadi kubwa ya watu waliokimbia makazi yao kutokana na mapigano katika maeneo mengine ya Sudan.
Soma zaidi:



















