Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Marekani yashambulia boti saba za Iran huko Hormuz

Operesheni hiyo ni sehemu ya mpango wa Marekani unaoitwa “Project Freedom”, ambao kwa mujibu wa Rais Trump unalenga kusaidia meli zilizokwama na wafanyakazi wake baharini kuondoka salama katika Mlango bahari wa Hormuz.

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga

  1. Rais wa Mali Goïta ajiteua kuwa Waziri wa Ulinzi

    Kiongozi wa kijeshi wa Mali, Meja Jenerali Assimi Goïta, amejiteua kushika nafasi ya Waziri wa Ulinzi, akiongeza wadhifa huo kwenye nafasi yake ya sasa ya Rais wa mpito.

    Hatua hiyo inafuatia kuuawa kwa aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, Sadio Camara, katika mashambulizi yaliyoratibiwa na wapiganaji wa JNIM pamoja na waasi wa Tuareg FLA. Camara alikuwa na mchanfgo mkubwa katika kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na Urusi, hivyo kifo chake ni pigo kubwa kwa jeshi la Mali.

    Kama Waziri wa Ulinzi, Goïta ambaye alitwaa madaraka kupitia mapinduzi ya kijeshi, sasa ataongoza moja kwa moja vyombo vya usalama akisaidiwa na Mkuu wa Majeshi ya nchi hiyo, Jenerali Oumar Diarra, aliyeteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Ulinzi.

    Mali kwa sasa inakabiliwa na ongezeko kubwa la mashambulizi na kupoteza maeneo kadhaa kwa makundi ya wapiganaji.

    Goïta aliingia madarakani mwaka 2020 akiwa na cheo cha kanali, kabla ya kupanda hadi kuwa Jenerali ndani ya miaka minne.

    Wachambuzi wanamkosoa wakisema hajafanikiwa kutimiza ahadi yake ya kurejesha usalama licha ya msaada wa kijeshi kutoka Moscow.

  2. Kilichojiri saa 24 zilizopita katika vita ya Iran

    Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) umesema Iran imefanya shambulio la kwanza la makombora na droni dhidi ya taifa hilo tangu kusitishwa kwa mapigano na Marekani kuanza Aprili 8, katika mfululizo wa matukio yanayoashiria kuongezeka tena kwa mvutano wa kijeshi katika Ghuba.

    Kwa mujibu wa taarifa za UAE, Iran ilirusha droni mbili dhidi ya meli iliyokuwa inapita katika Mlango wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.

    Katika upande mwingine, Jeshi la Marekani limesema limeendesha operesheni kali katika Mlango wa Hormuz, ambapo limeshambulia na kuziharibu boti saba ndogo za kijeshi za Iran zilizodaiwa kujaribu kuingilia usafirishaji wa meli zilizo chini ya ulinzi wa Marekani.

    Rais Donald Trump amesema operesheni hiyo ni sehemu ya mpango unaoitwa “Project Freedom” unaolenga kuhakikisha meli zinapita salama katika eneo hilo.

    Aidha, Marekani imeripoti kuwa meli mbili za kibiashara zilifanikiwa kupita salama katika Mlango wa Hormuz siku ya Jumatatu, zikilindwa na jeshi la Marekani, katika juhudi za kupunguza hatari kwa wafanyakazi wa baharini.

    Iran kwa upande wake imeendelea kusisitiza kuwa inadhibiti usalama wa Mlango wa Hormuz na imetishia kuzuia au kushambulia majeshi ya kigeni yanayojaribu kuingilia eneo hilo.

    Katika upande wa kidiplomasia, Tehran imesema imepokea jibu kutoka Marekani kuhusu pendekezo lake la amani lenye mambo 14, ambalo inalenga kumaliza vita. Hata hivyo, Trump amesema huenda akalikataa pendekezo hilo, akidai Iran “bado haijalipa gharama ya kutosha,” jambo linaloacha mustakabali wa mazungumzo ukiwa na mashaka makubwa.

  3. Iran yaishambulia UAE kwa droni na makombora 15

    Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), imesema imekumbwa na shambulio jipya kutoka Iran lililohusisha makombora 15 pamoja na ndege zisizo na rubani (droni), katika tukio linaloendelea kuongeza mvutano katika eneo la Ghuba.

    Kwa mujibu wa wizara ya ulinzi ya UAE, shambulio hilo lilijumuisha makombora 12 ya balistiki, makombora matatu ya cruise pamoja na droni nne. Watu watatu waliripotiwa kujeruhiwa kufuatia tukio hilo.

    UAE inasema mifumo yake ya ulinzi ilifanikiwa kudhibiti sehemu kubwa ya mashambulizi hayo kutoka Iran

    Taarifa hiyo imeongeza kuwa mifumo ya ulinzi wa anga ya nchi hiyo imekuwa ikikabiliana na mashambulizi hayo tangu kuanza kwa mgogoro wa Marekani na Iran Februari 28, ikidai kuwa imezuia jumla ya makombora 549 ya balistiki, makombora 29 ya cruise na zaidi ya droni 2,260.

  4. Iran yaubeza mpango wa Marekani wa 'Project Freedom' yasema hauna suluhisho

    Waziri wa mambo ya nje wa Iran Abbas Araghchi ameikosoa vikali operesheni ya Marekani iitwayo “Project Freedom”, akisema haina suluhisho la kijeshi na inaweza kuongeza mkwamo katika mgogoro unaoendelea katika Mlango wa Hormuz.

    Kupitia ujumbe wake kwenye mtandao wa X, Araghchi amesema matukio yanayoendelea Hormuz yanaonyesha wazi kuwa mgogoro huo ni wa kisiasa na hauwezi kutatuliwa kwa nguvu za kijeshi. Amesisitiza kuwa hatua za kijeshi zinaweza kuendeleza zaidi mzozo badala ya kuutatua.

    Kauli hiyo inakuja wakati mvutano ukiendelea kuongezeka kati ya Iran na Marekani, kufuatia mashambulizi ya hivi karibuni ya Marekani dhidi ya boti za Iran katika eneo hilo muhimu la usafirishaji wa mafuta duniani.

    Araghchi pia ameeleza kuwa mazungumzo ya kidiplomasia yanaanza kupata muelekeo kupitia juhudi za Pakistan, na kuitaka Marekani kutochochea mzozo mkubwa zaidi.

  5. Marekani yashambulia boti saba za kijeshi za Iran huko Hormuz

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema jeshi la nchi yake limeshambulia na kuziharibu boti saba ndogo za kijeshi za Iran katika Mlango bahari wa Hormuz, huku hali ya kijeshi katika njia hiyo muhimu ya usafirishaji duniani ikiendelea kuwa tete.

    Kwa mujibu wa taarifa za jeshi la Marekani, mashambulizi hayo yalitekelezwa kwa kutumia helikopta. Hata hivyo, Iran bado haijathibitisha wala kukanusha madai hayo.

    Operesheni hiyo ni sehemu ya mpango wa Marekani unaoitwa “Project Freedom”, ambao kwa mujibu wa Trump unalenga kusaidia meli zilizokwama na wafanyakazi wa baharini kuondoka salama katika Mlango wa Hormuz.

    Hata hivyo, Iran inaendelea kusisitiza kuwa mlango huo bado umefungwa na imedai kufyatua risasi za onyo dhidi ya manowari za Marekani, madai ambayo Washington imeyakanusha vikali.

    Operesheni hiyo ya kijeshi ya Marekani inahusisha meli za kivita na ndege zaidi ya 100 pamoja na wanajeshi takribani 15,000.

  6. Karibu katika habari zetu za moja kwa moja leo Mei 05, 2026