Polisi Tanzania inachunguza tukio la kutekwa kwa msaidizi wa Tundu Lissu
Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linasema kuwa linafuatilia taarifa ambazo zimekuwa zikienea katika mitandao ya kijamii zinazodai kutekwa kwa David Joseph Jumbe, Msaidizi wa Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chadema (Tundu Lissu) na watu wasiojulikana.
''Katika ufuatiliaji wa tukio hilo tulifanikiwa kupata gari nyeusi aina ya Toyota Wish ambalo Jumbe alikuwa ameabiri kabla ya kukamatwa na watu hao wasiojulikana,'' ilisema katika taarifa iliyotolewa muda mfupi uliopita.
Hapo awali Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara wa Amani Golugwa alitoa taarifa za kuthibitisha kupatikana kwa David Jumbe akiwa na pingu mikononi.
Golugwa aliongeza kuwa maafisa wa Jeshi la polisi walifika katika makao makao mkuu ya Chadema asubuhi ya leo Alhamisi na kusema kuwa wanamtafuta mtu anayedaiwa kutoroka akiwa na pingu.
''Walikuwa wanadai Jumbe amejificha ndani ya ofisi za Chadema na wanamtafuta ili wamfungue pingu,'' alisema Golugwa aliyenukuliwa na vyombo vya habari vya ndani.
Golugwa aliongeza kuwa aliwaambia askari hao kwamba Jumbe yuko nyumbani kwake wakamfungulie huko.
Baadaye mke wa Jumbe alithibitisha kuwa mume wake amerejea nyumbani.