Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Polisi Tanzania inachunguza tukio la kutekwa kwa msaidizi wa Lissu

Hapo awali Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara wa Amani Golugwa alitoa taarifa za kuthibitisha kupatikana kwa David Jumbe akiwa na pingu mikononi.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Beldeen Waliaula & Mariam Mjahid

  1. Polisi Tanzania inachunguza tukio la kutekwa kwa msaidizi wa Tundu Lissu

    Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linasema kuwa linafuatilia taarifa ambazo zimekuwa zikienea katika mitandao ya kijamii zinazodai kutekwa kwa David Joseph Jumbe, Msaidizi wa Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chadema (Tundu Lissu) na watu wasiojulikana.

    ''Katika ufuatiliaji wa tukio hilo tulifanikiwa kupata gari nyeusi aina ya Toyota Wish ambalo Jumbe alikuwa ameabiri kabla ya kukamatwa na watu hao wasiojulikana,'' ilisema katika taarifa iliyotolewa muda mfupi uliopita.

    Hapo awali Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara wa Amani Golugwa alitoa taarifa za kuthibitisha kupatikana kwa David Jumbe akiwa na pingu mikononi.

    Golugwa aliongeza kuwa maafisa wa Jeshi la polisi walifika katika makao makao mkuu ya Chadema asubuhi ya leo Alhamisi na kusema kuwa wanamtafuta mtu anayedaiwa kutoroka akiwa na pingu.

    ''Walikuwa wanadai Jumbe amejificha ndani ya ofisi za Chadema na wanamtafuta ili wamfungue pingu,'' alisema Golugwa aliyenukuliwa na vyombo vya habari vya ndani.

    Golugwa aliongeza kuwa aliwaambia askari hao kwamba Jumbe yuko nyumbani kwake wakamfungulie huko.

    Baadaye mke wa Jumbe alithibitisha kuwa mume wake amerejea nyumbani.

  2. DR Congo yafunga kambi ya mazoezi ya Kombe la Dunia kufuatia mlipuko wa Ebola

    Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo imefuta kambi yake ya mazoezi ya kabla ya Kombe la Dunia katika mji mkuu, Kinshasa, kufuatia mlipuko wa Ebola mashariki mwa nchi hiyo.

    Maandalizi ya timu ya taifa yamehamishiwa Ubelgiji huku maambukizi ya ugonjwa huo uliosababiisha vifo vya zaidi ya watu 130 ukiendelea yakiendelea kuenea.

    Shirika la Afya Dunianii (WHO) limetaja mlipuko huo kuwa "dharura ya afya ya kimataifa", lakini ilisema haijafikia kiwango cha janga.

    Jerry Kalemo, msemaji wa timu ya taifa ya kandanda, aliviambia vyombo vya habari vya kimataifa kuwa michezo ya kabla ya mashindano barani Ulaya itaendelea kama ilivyopangwa, huku kikosi kikiwa kinajiandaa kwa Kombe lao la kwanza la Dunia tangu 1974.

    DR Congo inatarajiwa kucheza mechi za kirafiki dhidi ya Denmark, tarehe 3 Juni nchini Ubelgiji, na Chile, Juni 9 nchini Uhispania, kabla ya kuelelkea kwa kipute cha Kombe la Dunia.

    Msemaji wa timu ya DR Congo aliliambia shirika la habari la Reuters kwamba kambi ya mazoezi ya kikosi hicho imevunjwa kutokana na vikwazo vya usafiri vilivyowekwa na Marekani, ambao ndio wenyeji wa Kombe la Dunia msimu huu wa joto, pamoja na Mexico na Canada.

    Shirika la afya ya umma la Marekani limepiga marufuku kuingia kwa watu wasio Wamarekani ambao wamekuwa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Uganda au Sudan Kusini katika siku 21 zilizopita, ili kukabiliana na mlipuko wa Ebola.

    Wachezaji wote wa DR Congo, pamoja na kocha wa timu hiyo Mfaransa, Sébastien Desabre, wako nchini Afrika ya kati na hawataathiriwa na vikwazo hivyo licha ya kambi ya mazoezi kufungwa.

    Maelezo zaidi:

  3. Raia 300 wa Ghana waondolewa Afrika Kusini kutokana na mashambulizi dhidi ya wahamiaji

    Raia 300 wa Ghana, wamejisajili na ubalozi wa taifa lao nchini Afrika Kusini, wakitaka kurejeshwa nyumbani baada ya kukumbana na chuki dhidi ya wahamiaji.

    Hatua hii ambayo imechukulia na wizara ya mambo ya kigeni ya Ghana, imejiri wakati kampeni ya chuki dhidi ya wahamiaji bado inashuhudiwa nchini Afrika Kusini.

    Kuanzia mwezi Aprili, wahamiaji wamekuwa wakikumbana na manyanyaso tofauti na vitisho kutoka kwa makundi yanayopinga wahamiaji nchini Afrika Kusini.

    Kampeni hiyo ya March and March Movement, inawakashifu wahamiaji kwa kuchukua nafasi za ajira za raia wa Afrika Kusini, pamoja na kuhusika na uhalifu.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Kushiriki mapenzi kwa kuridhiana kati ya vijana si hatia, mahakama ya Kenya yasema

    Mahakama moja nchini Kenya imetoa uamuzi kuwa baadhi ya vifungu vya sheria ya makosa ya unyanyasaji wa kingono nchini humo, haviwezi kutumika kwa watoto wanaopatikana wameshiriki mapenzi kwa kuridhiana.

    Watetezi wa haki wamesema uamuzi huo utasaidia kupunguza kukamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa vijana walioko chini ya umri wa miaka 18 wanaoshiriki mapenzi kwa kuridhiana na msichana pia aliyechini ya umri wa miaka 18.

    Uamuzi huo unatarajiwa kuleta mageuzi katika utendaji wa idara ya polisi, ikija katika suala la kuwaajibisha wanaoshtakiwa na kosa la unyanyasaji wa kingono pamoja na mageuzi katika utoaji wa huduma za afya ya uzazi kwa vijana.

    Uamuzi huo wa mahakama ya Kenya unasema kuwa, vijana waliobaleghe (mvulana na msichana) ambao umri wao unakaribiana hawafai kuchukuliwa hatua za kisheria moja kwa moja iwapo watapatikana wameshiriki mapenzi.

    Uamuzi huu unatokana na kesi mbili zilizokuwa katika mahakama, ambapo kijana mmoja mwenye umri wa miaka 17 alishtakiwa kumbaka msichana wa umri wa miaka 16, na nyingine kijana wa miaka 17 alishtakiwa kumpa uja uzito msichana mwenye umri sawa.

    Kulingana na sheria za Kenya, mtu aliye chini ya umri wa miaka 18, hana uwezo wa kujifanyia maamuzi ya kisheria.

    Pia unaweza kusoma:

  5. Waziri wa usalama wa ndani wa Israel akosolewa kwa kuwakejeli wanaharakati

    Jamii ya kimataifa imeilaani Israel, kwa kuwanyanyasa wanaharakati waliokuwa katika msafara wa Flotila uliokuwa ukipeleka misaada eneo la Gaza.

    Meli hizo zilizuiliwa na vikosi vya usalama wa bahari vya Israel.

    Marekani, Uingereza, Ufaransa, Italia na Canada ni miongoni mwa mataifa zilizo ghadhabishwa na hatua ya Waziri wa Usalama wa ndani wa Israel, Itamar Ben-Gvir, ya kuchapisha video ikimuonesha akiwakejeli wanaharakati waliokuwa wamepiga magoti, wakiwa wamefungwa mikono nyuma ya mgongo.

    Kundi la kutetea haki za binadamu linalowakilisha watu hao 430 kutoka zaidi ya mataifa 40, waliokuwa katika msafara wa Global Sumud Flotilla linataka wanaharakati hao waachiliwe huru.

    Pia unaweza kusoma:

  6. Mitandao ya Tiktok na Youtube si salama kwa watoto, yasema ripoti ya Ofcom

    Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano nchini Uingereza Ofcom, imekosoa mitandao ya TikTok na YouTube katika ripoti yake na kusema kuwa, mifumo ya maudhui ya mitandao hiyo si salama kwa watoto.

    Mamlaka hiyo inataka mitandao hiyo kuweka udhibiti mkali kuhusu usalama wa watoto mitandaoni.

    Kampuni za Meta, Snap na Roblox, zimesema zitashughulikia mapendekezo waliyopewa na kuweka udhibiti mkali, ili watoto wasikutane na maudhui ambayo hayafai mitandaoni.

    Uingereza bado inajadili sheria ya kuwazuia watoto chini ya umri wa miaka 16, kutotumia mitandao ya kijamii.

    Kwa kujibu ripoti ya Ofcom, TikTok na YouTube zimesisitiza kuhusu vipengele vya usalama vilivyopo kwenye mitandao yao, ikiwemo TikTok kuzuia kutuma ujumbe wa moja kwa moja kwa watoto chini ya miaka 16, na YouTube kuweka kipengele cha muda wa kutazama video fupi (Shorts), kinachowaruhusu wazazi kuweka muda wa matumizi wa mtandao huo kwa watoto.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Kuilazimisha Iran kujisalimisha ni 'ndoto ya mchana'

    Katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa kijamii wa X, Rais wa Iran Masoud Pezeshkian, aliandika kuwa kuilazimisha Iran ijisalimishe ni “ndoto ya mchana.”

    Rais huyo aliongezea kuwa “Iran imekuwa ikizingatia kwa uaminifu ahadi zake na imetumia kila njia ya kuzuia vita”

    “Kuilazimisha Iran kujisalimisha ni ndoto ya mchana, na lazima kuwe na heshima katika njia zote za diplomasia zinazotumika ili kupata amani ya kudumu”

    Kauli ya Pezeshkian inajiri wakati Rais wa Marekani Donald Trump,alidokeza kuwa mazungumzo na Iran yako katika hatua za mwisho, na kuonya kuwa mashambulizi zaidi yanaweza kutekelezwa ikiwa Tehran haitakubali kuafikia makubaliano.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Marekani imemfungulia mashtaka kiongozi wa zamani wa Cuba Raul Castro

    Marekani imemshtaki kiongozi wa zamani wa Cuba, Raul Castro, kwa kupanga kuwaua raia wa Marekani na makosa mengine yaliyotokana na kuangushwa kwa ndege mbili zilizokuwa zikifanya safari kutoka eneo la Florida hadi Cuba.

    Kesi hiyo inamshtumu Castro na watu wengine watano kwa kuzifyatulia risasi ndege hizo, zilizokuwa zinamilikiwa na kundi la Cuba-America Group Brothers, na kuwauwa watu wanne, watatu wakiwa raia wa Marekani.

    Castro, kwa sasa ana umri wa miaka 94, na wakati huo alikuwa mkuu wa majeshi ya Cuba na alikashifiwa vikali kimataifa baada ya tukio hilo.

    Wakati Marekani inaendelea kuongeza shinikizo dhidi ya utawala wa kikomunisti wa Cuba, Rais Miguel Díaz-Canel ameelezea mashtaka hayo kama “shinikizo la kisiasa, usio na msingi wa kisheria.”

    Akizungumza katika jengo la Freedom Tower mjini Miami, Mwanasheria Mkuu wa Marekani Todd Blanche, alitangaza kuwa taifa lake litamfungulia Castro mashtaka ya uharibifu wa ndege na makosa manne ya mauaji .

    “Marekani, na Rais Trump, haisahau wala haitasahau raia wake,” Blanche alisema.

    Mashtaka hayo yataskizwa katika mahakama za Marekani, na kila shtaka la mauaji linaweza kuwa na adhabu ya kifo au kifungo cha maisha.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Trump asema atazungumza na kiongozi wa Taiwan, hatua inayovunja utaratibu wa kidiplomasia

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema atazungumza na kiongozi wa Taiwan, Lai Ching-te, kuhusu uwezekano wa kuiuzia Taiwan silaha, hatua ambayo ni mabadiliko makubwa kutoka utamaduni wa kidiplomasia uliodumu kwa miaka mingi katika kisiwa hicho na Marekani.

    Viongozi wa Marekani na Taiwan hawajawahi kuzungumza moja kwa moja tangu mwaka wa 1979, wakati Washington ilipositisha rasmi uhusiano wake na Taiwan ili kuitambua serikali ya Beijing kama serikali halali ya China.

    Beijing inaichukulia Taiwan kama sehemu ya himaya yake na haijaondoa uwezekano wa kuitwaa kwa nguvu za kijeshi.

    Lai, aliingia madarakani mwaka wa 2024, na ameongoza moja ya juhudi kubwa zaidi katika miaka ya hivi karibuni za kuimarisha ulinzi wa kisiwa hicho.

    Marekani kwa muda mrefu imekuwa ikiunga mkono Taiwan na kuipatia silaha za kujilinda, lakini imekuwa ikijaribu kudumisha uhusiano wa kidiplomasia na China.

    Alipoulizwa na wanahabari iwapo anapanga kuzungumza na Lai, kuhusu kuiuzia Taiwan silaha, Trump alisema, “nitazungumza naye. Nazungumza na kila mtu tutalifanyia kazi hilo, tatizo la Taiwan.”

    Katika ziara yake ya hivi karibuni nchini China, Rais Xi Jinping wa China alitaka Marekani kusitisha uuzaji wa silaha kwa Taiwan.

    Mwaka wa 1979, Marekani ilipitisha Sheria ya Mahusiano na Taiwan inayoruhusu Marekani kuipatia Taiwan silaha za kujilinda, sheria ambayo inatumika kuiuzia Taiwan silaha hadi leo.

    Pia unaweza kusoma:

  10. Chanjo ya Ebola huenda ikachukua miezi tisa, WHO yaonya

    Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema huenda ikachukua hadi miezi tisa kabla ya chanjo dhidi ya aina ya Ebola inayosambaa kwa sasa kuwa tayari.

    Chanjo mbili ambazo zinazoweza kutumika dhidi ya Ebola ya Bundibugyo zinatengenezwa, lakini hakuna hata moja ambayo imefanyiwa majaribio ya kitabibu kufikia sasa,hii ni kulingana na mshauri wa shirika la WHO, Dkt Vasee Moorthy.

    Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Adhanom, amesema kumekuwa na visa 600 vya Ebola na vifo 139 kutokana na ugonjwa huo, huku idadi hiyo ikitarajiwa kuongezeka.

    WHO ilitangaza hali ya dharura ya afya ya umma ya kimataifa, lakini ikasema hali hiyo bado haijafikia kiwango cha kuwa janga la dunia.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Trump: Mazungumzo na Iran yako katika hatua za mwisho, tutawashambulia iwapo hawataafikia makubaliano

    Rais wa Marekani Donald Trump, amesema kuwa wapo katika hatua za mwisho za mazungumzo ya kupatikana kwa amani na Iran, na wasipoafikia makubaliano, wataanzisha wimbi jipya la mashambulizi.

    Wiki sita sasa tangu kusitishwa kwa oparesheni ya “epic fury” mazungumzo ya kumaliza vita hivyo hayajapiga hatua kubwa.

    Trump alisema wiki hii, karibu atoe agizo la kutekeleza mashambulizi zaidi, ila aliombwa asifanye hivyo na mataifa ya Ghuba ili kutoa nafasi kwa mazungumzo kufanyika.

    “Tuko katika hatua za mwisho za mazungumzo na Iran. Tutaona kile ambacho kitatokea baadaye. Tutaafikiana au tutafanya vitu ambavyo si vizuri, ila nadhani hatutafika huko” Trump aliwaambia wanahabari.

    Rais huyo aliongezea kuwa “tunawapa nafasi, sina haraka. Ni heri watu wachache kuuawa kuliko watu wengi. Mkondo wowote unaweza kuchukuliwa”

    Serikali ya Iran nayo imemkosoa vikali Trump kwa kutaka kuanzisha tena vita hivyo, na kusema kuwa wako tayari kuanzisha mashambulizi yatakayokwenda nje ya eneo la Mashariki ya Kati.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja Alhamisi ya leo.