Moja kwa moja, Rais wa Uganda aapishwa kwa muhula wa saba mfululizo

Ulinzi mkali, ikiwa ni pamoja na vifaru vya kivita, uliwekwa katika mji mkuu, Kampala,.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid & Asha Juma

  1. Ufaransa inatafuta uhusiano zaidi ya wa kikoloni na viongozi wa Afrika

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Ikishutumiwa kwa ukoloni mamboleo kuingilia kati katika nchi nyingi za Afrika ambapo kwa kawaida imekuwa na uhusiano wa karibu, Ufaransa inapanua wigo wake kwa kuandaa mkutano wa viongozi wa Afrika nchini Kenya inayozungumza Kiingereza kwa mara ya kwanza.

    Akizungumza katika Mkutano wa Afrika ulioandaliwa katika mji mkuu wa Nairobi siku ya Jumanne, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alizungumzia mara kwa mara kuhusu "uwekezaji wa pamoja" na "ushirikiano sawa" alipoelezea changamoto zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na usalama, utegemezi wa kiuchumi na ushindani wa kijiografia.

    Rais wa Kenya William Ruto, ambaye ni mwenyeji mwenza wa mkutano huo wa siku mbili, alishirikisha hisia zake, akiongeza kuwa Afrika lazima isaidie kuunda utaratibu unaoibuka wa kimataifa badala ya kubaki pembezoni mwake.

    Macron ametangaza uwekezaji wenye thamani ya dola bilioni 27 (pauni bilioni 20) barani Afrika katika maeneo kama vile mpito wa nishati, kidijitali na akili mnemba, uchumi wa baharini na kilimo.

    "Afrika inafanikiwa. Ni bara changa zaidi duniani ... na inahitaji uwekezaji ili kujitegemea zaidi," alisema Jumatatu, akiongeza kuwa hii itaunda ajira zipatazo 250,000 barani Afrika, na nchini Ufaransa.

    "Hatuko hapa tu kuja kuwekeza katika bara la Afrika pamoja nanyi - tunahitaji viongozi wakubwa wa biashara wa Kiafrika kuja kuwekeza nchini Ufaransa," aliwaambia wasikilizaji katika kituo cha mikutano cha Nairobi, shirika la habari la AFP linaripoti.

    Mkutano huo unalenga kupanua ushirikiano wa Paris na kufanya mikataba ya uwekezaji barani humo dhidi ya kuongezeka kwa hisia za chuki dhidi ya Ufaransa na kupungua kwa mamlaka katika makoloni yake ya zamani, hasa Afrika Magharibi. Hii inaonyesha mabadiliko ya hatua kwa hatua katika jinsi Paris inavyofikiria uhusiano wake na Afrika.

  2. Rais wa Uganda aapishwa kwa muhula wa saba mfululizo

    .

    Chanzo cha picha, Government of Uganda/X

    Rais wa Uganda Yoweri Museveni, mwenye umri wa miaka 81, ameapishwa kwa muhula wa saba mfululizo baada ya ushindi wake mkubwa katika uchaguzi uliopingwa mnamo mwezi Januari, na kuongeza muda wake kama mmoja wa watawala waliohudumu kwa muda mrefu zaidi barani Afrika.

    Ulinzi mkali, ikiwa ni pamoja na vifaru vya kivita, uliwekwa katika mji mkuu, Kampala, kabla ya kuapishwa kwake katika kile polisi walisema ni hatua zinazolenga kudumisha utulivu wa umma.

    Museveni alitangazwa mshindi wa uchaguzi huo kwa zaidi ya asilimia 70 ya kura, huku muhula wake ukitarajiwa kuisha mwaka wa 2031.

    Mpinzani wake mkuu, nyota wa pop aliyegeuka kuwa mwanasiasa Bobi Wine, alikataa matokeo, akisema kura hiyo ilikumbwa na "udanganyifu". Maafisa wa uchaguzi walikanusha madai hayo.

    Kiongozi huyo wa upinzani mwenye umri wa miaka 44, ambaye jina lake halisi ni Robert Kyagulanyi Ssentamu, alikimbia nchi baada ya uchaguzi, akisema anaogopa kwamba "utawala ulitaka kuniangamiza".

    Museveni aliingia madarakani kwa mara ya kwanza kama kiongozi wa waasi mwaka 1986 lakini tangu wakati huo ameshinda chaguzi saba.

    Yeye ni miongoni mwa viongozi wachache wa Afrika walio madarakani kwa zaidi ya miaka 40. Wengine ni pamoja na Denis Sassou Nguesso wa Congo-Brazzaville, Teodoro Obiang wa Equatorial Guinea na Paul Biya wa Cameroon.

    Sherehe ya kuapishwa ilifanyika katika Viwanja vya Uhuru vya Kololo jijini Kampala. Serikali ilitangaza siku hiyo kuwa sikukuu ya umma.

    Soma zaidi:

  3. Tukishambuliwa tutarutubisha urani kwa kiwango cha silaha - Iran

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Iran imesema inaweza kuongeza kiwango cha urutubishaji wa urani hadi asilimia 90 iwapo itashambuliwa tena, hatua inayoweza kuongeza mvutano katika eneo la Mashariki ya Kati.

    Kauli hiyo imetolewa na msemaji wa kamati ya usalama wa taifa ya bunge la Iran, Ebrahim Rezaei, aliyesema suala hilo linaweza kujadiliwa rasmi bungeni.

    Asilimia 90 ya urutubishaji urani hutajwa kuwa kiwango kinachoweza kutumika kutengeneza silaha za nyuklia, huku Iran kwa sasa ikidaiwa kuwa tayari imefikia asilimia 60.

    Onyo hilo limekuja baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kusema makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Iran yako katika hali tete.

    Marekani na Israel ziliwahi kushambulia vituo vya nyuklia vya Iran mwaka jana, lakini bado kuna sintofahamu kuhusu akiba ya urani yenye kiwango cha juu iliyobaki nchini humo.

    Mashirika ya ujasusi ya Marekani yanaamini mpango wa nyuklia wa Iran utaendelea kuwa tishio iwapo akiba hiyo haitaharibiwa au kuondolewa.

  4. Mfanyabiashara wa dhahabu wa Tanzania akamatwa kwa mauaji ya mwanafunzi wa Chuo Kikuu Kenya

    Ni picha ya Alice Rian'ga aliyeuawa na kutupwa msituni

    Chanzo cha picha, Socials

    Maelezo ya picha, Ni picha ya Alice Rian'ga aliyeuawa na kutupwa msituni

    Maximillian John Madeni, mfanyabiashara wa dhahabu kutoka Tanzania, amekamatwa kuhusiana na mauaji yanayoshukiwa ya mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Jaramogi Oginga Odinga idara ya sayansi na teknolojia katika eneo la Bondo nchini Kenya.

    Mwili wa mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 20, aliyekuwa akisomea Shahada ya Elimu ya Sayansi mwaka wa pili, ulipatikana Jumamosi katika eneo la Barkowino ndani ya mji wa Bondo, Kaunti ya Siaya.

    Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Bondo huko Kenya, Robert Aboki, amesema mwili huo uligunduliwa na wanawake waliokuwa wakikusanya kuni kabla ya kutoa taarifa kwa mamlaka husika.

    Polisi wamesema marehemu, Alice Rianga, alionekana mara ya mwisho Jumatano iliyopita alipoondoka katika chumba chake mjini Bondo kuelekea chuo hicho lakini hakurejea.

    Maafisa wa upelelezi walisema eneo ambalo mwili wa mwanafunzi huyo ulipatikana haukuwa na dalili za mapambano ya kimwili, jambo linaloashiria kuwa huenda aliuawa sehemu nyingine kabla ya mwili wake kutupwa kichakani.

    Wachunguzi pia walibaini kuwa mwili huo ulikutwa bila nguo za ndani.

    Kwa mujibu wa chombo cha habari cha Kenya, Citizen TV, Mwenza wake wa chumbani, Kayla Wanyonyi, alitoa taarifa ya kupotea kwake Jumapili iliyofuata, ambapo maelezo aliyotoa yalilingana na mwili uliokuwa umepatikana siku moja kabla.

    Uchunguzi wa awali umehusisha Madeni na tukio hilo baada ya Kayla Wanyonyi kumtaja kuwa mpenzi wa marehemu.

    Mwili wa mwanafunzi huyo kwa sasa umehifadhiwa katika mochari ya Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Bondo ukisubiri kufanyiwa uchunguzi wa maiti, huku polisi wakiendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo chake.

    Soma zaidi:

  5. Pakistan yakanusha madai kuwa inawahifadhia kwa siri ndege za kijeshi za Iran

    h

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Pakistan imekanusha vikali madai yaliyotolewa na kituo cha televisheni cha Marekani CBS News, ikiyataja kuwa “yasiyo na msingi, ya kusisimua kupita kiasi na yanayopotosha”, kwamba nchi hiyo iliwapa hifadhi ndege za kijeshi za Iran ili kuzilinda dhidi ya mashambulizi yanayoweza kufanywa na Marekani kufuatia usitishaji mapigano wa hivi karibuni kati ya Iran na Marekani.

    Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan imesema: “Inaonekana kuwa uvumi kama huu unalenga kudhoofisha juhudi zinazoendelea za kuleta utulivu na amani ya kikanda.”

    CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani, ilidai katika ripoti yake ya Mei 11, ikinukuu maafisa wa Marekani, kwamba ndege kadhaa za Iran, zikiwemo ndege aina ya RC 130, zilipelekwa katika Kituo cha Anga cha Nur Khan kilichopo Rawalpindi mapema mwezi Aprili.

    Ripoti hiyo inadai kuwa “Pakistan, wakati ikijionyesha kama mpatanishi wa kidiplomasia kati ya Tehran na Washington, iliruhusu kwa siri ndege za kijeshi za Iran kuegeshwa katika viwanja vyake vya anga, hatua ambayo huenda ililenga kuzilinda dhidi ya mashambulizi ya anga ya Marekani.”

    CBS, ikinukuu maafisa wa Marekani ambao hawakutajwa majina, ilidai kuwa “Tehran ilipeleka ndege kadhaa katika Kituo cha Anga cha Jeshi la Anga la Pakistan cha Nur Khan siku chache baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kutangaza usitishaji mapigano na Iran mapema Aprili.”

    Pia unaweza kusoma:

  6. Lamine Yamal aibeba bendera ya Palestina wakati wa sherehe za ubingwa wa Barcelona

    Yamal

    Chanzo cha picha, INSTAGRAM/Reuters

    Maelezo ya picha, Nyota wa soka wa Hispania na duniani, Lamine Yamal akiwa anaipeperusha bendera

    Nyota wa soka wa Hispania na duniani, Lamine Yamal, ambaye Jumapili usiku aliiwezesha FC Barcelona kutwaa ubingwa wa La Liga baada ya kuifunga Real Madrid katika mchezo wa El Clásico, alijipata kwenye vichwa vya habari Jumatatu baada ya kuonekana akiinua bendera ya Palestina wakati wa sherehe za ushindi mitaani.

    Barcelona iliifunga Real Madrid mabao 2-0 katika mechi yake ya mwisho, na hivyo kuthibitisha ubingwa wake ikiwa zimesalia wiki tatu kumalizika kwa msimu, na kutwaa ubingwa wa klabu wa Hispania kwa mara ya 29.

    Hispania ni miongoni mwa nchi zinazoongoza katika Umoja wa Ulaya katika kuitambua Palestina kama taifa huru.

    Soma zaidi:

  7. Starmer akabiliwa na shinikizo la kujiuzulu baada ya zaidi ya wabunge 70 wa Labour kumkataa

    h

    Chanzo cha picha, PA Media

    Zaidi ya wabunge 70 wamemtaka Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, kujiuzulu kufuatia shinikizo kubwa ndani ya chama chake cha Labour baada ya matokeo mabaya katika uchaguzi wa serikali za mitaa nchini Uingereza.

    Kiongozi huyo wa chama tawala cha Labour anakabiliwa na shinikizo kubwa kutoka ndani ya chama chake mwenyewe, ambapo idadi ya wabunge wa Labour wanaomtaka aachie ngazi imevuka 70.

    Katika moja ya siku ngumu zaidi tangu aingie madarakani, Starmer anatarajiwa kuongoza kikao cha baraza la mawaziri leo.

    Hata hivyo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Shabana Mahmood, ambaye pia ni mwanachama wa baraza la mawaziri, yumo miongoni mwa wanaomwomba Starmer ajiuzulu.

    Mbunge wa Labour, Jonathan Hinder, ambaye pia alitoa wito wa kujiuzulu kwake, alisema: “Hakuna waziri mkuu anayeweza kuendelea hivi. Ni wakati wa kuwa wakweli, anaondoka.”

    Akizungumza na BBC, Hinder alisema: “Tunahitaji kiongozi mpya wa Chama cha Labour, na muhimu zaidi, nchi yetu inahitaji kiongozi mpya.”

    Tarehe 11 Mei, Waziri Mkuu Starmer alitoa hotuba iliyolenga kupunguza shinikizo la kisiasa lililokuwa likiongezeka, akisisitiza kuwa hatajiuzulu. Alikiri kuwa serikali imefanya makosa, lakini akasisitiza kuwa imechukua “maamuzi sahihi makubwa ya kisiasa”.

    “Ninajua wapo wanaonitilia shaka, na najua lazima nizithibitishe hizo shaka kuwa si sahihi, na nitafanya hivyo,” alisema akijaribu kutoa ujumbe wa utulivu.

    Starmer pia aliahidi kurejesha uhusiano wa karibu na Ulaya.

    Mwandishi mwandamizi wa masuala ya kisiasa wa BBC, Chris Mason, aliyekuwa akifuatilia mjadala huo, alisema kuwa mvutano wa Starmer ulionekana wazi.

    Katika makala yake ya baadaye, aliripoti kuwa mawaziri wa baraza lake la mawaziri “wamegawanyika” kuhusu mustakabali wake.

    Mason aliandika: “Inaonekana bwawa sasa limevunjika. Wabunge wengi wa Labour wanasema wamepoteza imani na Waziri Mkuu kiasi kwamba ni vigumu kufuatilia idadi yao.”

    Chama cha Labour kilichoshika madaraka kwa wingi wa wabunge mwezi Julai 2024, kilipoteza takriban viti 1,500 vya halmashauri katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika Mei 7, 2026.

    Kwa upande mwingine, chama cha Reform UK kilichopinga uhamiaji kilipata mafanikio makubwa katika ngome za Labour.

    Chama hicho pia kilikumbwa na kipigo cha kihistoria nchini Wales, kikishindwa kwa mara ya kwanza baada ya takriban miaka 100.

    Katika kipindi chake cha miaka miwili madarakani, serikali ya Starmer imekumbwa na changamoto katika kutimiza ahadi za ukuaji wa uchumi, kuboresha huduma za umma, kurekebisha mfumo wa ustawi wa jamii na kupunguza gharama za maisha.

    Soma pia:

  8. Pakistan yashutumiwa kuhifadhi kwa siri ndege za kijeshi za Iran katika vituo vyake vya anga

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani, limeripoti kuwa Pakistan imekuwa “ikihifadhi kwa siri” baadhi ya ndege za kijeshi za Iran.

    Kwa mujibu wa ripoti hiyo, ikiwanukuu maafisa wawili wa Marekani, Pakistan imewaruhusu Iran kuweka baadhi ya ndege zake za kijeshi katika vituo vyake vya anga katika kipindi ambacho juhudi za kusitisha vita kati ya Iran na Marekani zinaendelea. Maafisa hao walisema hatua hiyo inaweza kuonyesha kuwa Iran ililenga kuzilinda ndege zake dhidi ya mashambulizi ya anga ya Marekani.

    Maafisa hao pia waliiambia CBS News kwamba Iran imepeleka baadhi ya ndege za kiraia nchini Afghanistan, ingawa bado haijathibitishwa kama baadhi ya ndege hizo zilikuwa za kijeshi.

    Kwa mujibu wa taarifa hizo, hatua hizo zinaonyesha jitihada za Tehran kuokoa baadhi ya mali zake za kijeshi na za anga dhidi ya kuenea kwa mgogoro huo, huku Pakistan ikijitangaza hadharani kuwa mpatanishi katika kupunguza mvutano.

    Maafisa wa Marekani waliotoa taarifa hizo kwa CBS kwa masharti ya kutotajwa majina walisema kuwa siku chache baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kutangaza usitishaji mapigano na Iran mapema Aprili, Tehran ilihamisha baadhi ya ndege zake kwenda Kituo cha Anga cha Noor Khan, kilicho karibu na mji wa kijeshi wa Rawalpindi.

    CBS iliripoti kuwa miongoni mwa vifaa vilivyohamishwa ni ndege ya kijeshi ya Iran aina ya RC 130 Hercules, ambayo hutumika kwa upelelezi na ukusanyaji wa taarifa za kijeshi, ikiwa ni toleo maalum la ndege ya Lockheed C 130 Hercules.

    Kwa upande wake, Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani ilielekeza maoni yake kwa mamlaka za Afghanistan na Pakistan.

    Hata hivyo, afisa mmoja mwandamizi wa Pakistan amepinga madai hayo kuhusu kituo cha Noor Khan, akiiambia CBS News kuwa kituo hicho kiko katikati ya mji na haiwezekani kuficha kundi kubwa la ndege za kijeshi bila kuonekana na umma.

    Soma zaidi:

  9. Iran yasema hakuna mbadala wa kukubali masharti yake ya kusitisha vita na Marekani

    Ghalibaf

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelezo ya picha, Glalibaf ni kiongozi wa Iran aliye na ushawishi mkubwa nchini humo.

    Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Bagher Ghalibaf, amesema hakuna njia nyingine isipokuwa kukubali haki za wananchi wa Iran kama zilivyoainishwa katika pendekezo la vipengele 14 lililowasilishwa na Tehran.

    Kauli hiyo ilichapishwa Jumatatu jioni kupitia akaunti yake kwenye mtandao wa X kwa lugha ya Kiingereza, ambapo alisema: “Njia nyingine yoyote haitakuwa na matokeo na italeta kushindwa mfululizo pekee. Kadri wanavyoendelea kuchelewesha, ndivyo walipa kodi wa Marekani watakavyoendelea kubeba gharama kubwa zaidi.”

    Awali, Ghalibaf alikuwa amesema katika ujumbe mwingine kuwa Iran iko tayari kwa hali yoyote itakayojitokeza.

    Matamshi hayo yanaonekana kuwa majibu kwa kauli za Rais wa Marekani, Donald Trump, ambaye alionyesha kutoridhishwa kwake na majibu ya Iran kuhusu mapendekezo ya Marekani ya kumaliza mzozo huo.

    Trump alisema Jumatatu kuwa usitishaji mapigano kati ya Marekani na Iran uko katika hali ya “kutegemea mashine ya kupumulia”, akimaanisha kuwa makubaliano hayo yako katika hali dhaifu kutokana na kutoridhishwa kwake na msimamo wa Tehran.

    Pia unaweza kusoma:

  10. UAE yahusishwa na mashambulizi ya siri dhidi ya Iran - Jarida la Wall Street

    D

    Chanzo cha picha, EPA/Shutterstock

    Gazeti la The Wall Street Journal limeripoti kuwa U.A.E imekuwa ikihusika kwa siri katika mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Iran, kwa mujibu wa vyanzo vilivyoelezwa kuwa na taarifa kuhusu suala hilo.

    Iwapo taarifa hiyo itathibitishwa rasmi, inaweza kuifanya UAE kuwa miongoni mwa mataifa yanayoshiriki moja kwa moja katika mzozo unaoendelea dhidi ya Iran.

    Chanzo kimoja kilichozungumza na Wall Street Journal kilisema mashambulizi hayo, ambayo UAE haijayathibitisha rasmi, yalihusisha shambulizi dhidi ya kiwanda cha kusafisha mafuta kwenye kisiwa cha Labuan katika Ghuba ya Uajemi.

    Mapema mwezi Aprili, wakati ambapo Rais wa Marekani, Donald Trump, alikuwa akitangaza usitishaji mapigano, mashambulizi ya anga pia yaliripotiwa kulenga miundombinu ya mafuta ya Iran kwenye visiwa na maeneo ya baharini yanayomilikiwa na Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Iran.

    Mashambulizi hayo yalisababisha moto mkubwa na kuharibu sehemu kubwa ya mtambo wa Lavan, hali iliyotarajiwa kuathiri shughuli zake kwa miezi kadhaa.

    Baadaye Iran ilisema mtambo huo ulikuwa umelengwa na “shambulizi la adui”, kabla ya kujibu kwa kurusha makombora na ndege zisizo na rubani kuelekea UAE na Kuwait.

    Ripoti hiyo pia ilisema kuwa Marekani haikuonyesha wasiwasi mkubwa kuhusu mashambulizi hayo, kwa kuwa usitishaji mapigano ulikuwa bado haujatekelezwa kikamilifu.

    Wall Street Journal iliongeza kuwa Washington “iliupokea vyema ushiriki wa UAE” katika operesheni hizo.

    Soma zaidi:

  11. Marekani yafanya mazungumzo ya siri kufungua kambi mpya za kijeshi Greenland

    Makamu wa Rais JD Vance alitembelea kambi pekee ya jeshi la Marekani kwenye eneo hilo mapema mwaka huu.

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Makamu wa Rais JD Vance alitembelea kambi pekee ya jeshi la Marekani kwenye eneo hilo mapema mwaka huu.

    Marekani imekuwa ikifanya mazungumzo ya siri na Denmark kuhusu kupanua uwepo wake wa kijeshi nchini Greenland, kwa mujibu wa maafisa kadhaa wanaofahamu majadiliano hayo, huku mazungumzo kati ya pande hizo yakiripotiwa kupata mafanikio katika miezi ya hivi karibuni.

    Maafisa wa Marekani wanataka kufungua kambi tatu mpya za kijeshi kusini mwa Greenland, eneo lenye mamlaka ya kujitawala chini ya Denmark, wakati wakijaribu kutuliza mvutano wa kidiplomasia uliosababishwa na Rais wa Marekani, Donald Trump, baada ya kutishia kuichukua Greenland kwa nguvu.

    Kambi hizo zinatarajiwa kujengwa kusini mwa Greenland na zitajikita zaidi katika ufuatiliaji wa shughuli za majini zinazoweza kufanywa na Urusi na China katika eneo la Atlantiki ya Kaskazini kati ya Greenland, Iceland na Uingereza, eneo linalojulikana kama GIUK Gap.

    Ikulu ya White House imethibitisha kuwa serikali ya Marekani inaendelea na mazungumzo ya ngazi ya juu na Greenland pamoja na Denmark, lakini imekataa kutoa maelezo zaidi kuhusu majadiliano hayo.

    Denmark hapo awali ilionyesha utayari wa kujadili uwezekano wa kuongezwa kwa kambi za kijeshi za Marekani nchini Greenland, huku Wizara yake ya Mambo ya Nje ikithibitisha kuwa mazungumzo hayo yanaendelea.

    “Kuna mazungumzo ya kidiplomasia yanayoendelea na Marekani. Wizara ya Mambo ya Nje haitatoa maelezo zaidi kwa sasa,” msemaji wa wizara hiyo alisema.

    Vyanzo hivyo vimesema bado hakuna makubaliano rasmi yaliyofikiwa na idadi ya mwisho ya kambi inaweza kubadilika. Moja ya kambi hizo huenda ikajengwa Narsarsuaq katika eneo la zamani lililokuwa na kambi ya kijeshi ya Marekani pamoja na uwanja mdogo wa ndege.

    Hata hivyo, maafisa wa Marekani hawajazungumzia uwezekano wa kuichukua Greenland kwa nguvu wakati wa mazungumzo hayo, jambo ambalo Denmark na muungano wa kijeshi wa NATO wamekuwa wakilipinga hadharani.

    Kwa sasa, Marekani ina kambi moja pekee ya kijeshi Greenland, tofauti na takriban vituo 17 vya kijeshi vilivyokuwepo wakati wa Vita Baridi. Kambi hiyo ya Pituffik Space Base iliyopo kaskazini magharibi mwa Greenland hutumika kufuatilia makombora kwa ajili ya NORAD, lakini haijajengwa kwa ajili ya ufuatiliaji wa shughuli za majini.

    Baadhi ya maafisa wa sasa na wa zamani pamoja na wataalamu wa usalama wa eneo la Arctic wameiambia BBC kuwa Washington ingeweza kusukuma maslahi yake Greenland bila kutoa vitisho vikali dhidi ya mshirika wake wa NATO.

    “Kwanini umtishie mshirika kwa operesheni ya kijeshi au uvamizi wakati kile unachotaka kinaweza kujadiliwa kwa urahisi?” alisema afisa mmoja wa zamani mwandamizi wa ulinzi wa Marekani.

    Trump alionesha nia ya kuipa Marekani ushawishi mkubwa Greenland tangu muhula wake wa kwanza madarakani, lakini kauli zake za hivi karibuni zimezua mvutano wa kidiplomasia na kuangazia tofauti ndani ya NATO kuhusu msimamo wa serikali yake.

    Soma Pia:

  12. Trump asema usitishaji mapigano kati ya Marekani na Iran uko katika 'hali mahututi'

    g

    Chanzo cha picha, Bloomberg via Getty Images

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema usitishaji mapigano wa mwezi mmoja kati ya Marekani na Iran uko katika “hali mahututi sana”.

    Akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi ya Oval Jumatatu, Trump amesema ingawa usitishaji huo bado upo, umeendelea kuwa “dhaifu kupita kiasi”.

    “Ningesema usitishaji mapigano uko katika hali mahututi sana. Ni kama daktari anapoingia na kusema mgonjwa ana nafasi ya asilimia moja pekee ya kuendelea kuishi,” amesema.

    Trump pia amewashutumu viongozi wa Iran kwa kuwa “wasiokuwa waaminifu”, akisema wamebadilisha msimamo mara kadhaa katika mazungumzo.

    “Huo upuuzi waliotutumia hata sikuumaliza kuusoma,” alisema.

    Aidha, Trump ameishutumu Iran kwa kuvunja makubaliano ya kuruhusu Marekani kuondoa akiba yake ya urani iliyorutubishwa, huku akisisitiza kuwa Iran “haitawahi kuwa na silaha za nyuklia”.

    Kauli hiyo imekuja baada ya Iran kuwasilisha mapendekezo yake ya kumaliza vita na kufunguliwa tena kwa Mlango wa Hormuz kupitia ofa mbadala iliyotumwa kwa Marekani Jumapili. Trump aliyakataa mapendekezo hayo, akiyataja kuwa “hayakubaliki kabisa” na “upuuzi mtupu”.

    Kufuatia matamshi ya Trump, Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Ghalibaf, aliandika kwenye mtandao wa X kwamba majeshi ya Iran yako “tayari kujibu na kutoa funzo kwa uchokozi wowote”.

    Kwa upande wake, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alisema mapendekezo ya Tehran yalikuwa ya “uwajibikaji” na “ukarimu”.

    Baadaye, Ghalibaf alisema katika ujumbe mwingine kuwa “hakuna njia nyingine isipokuwa kukubali haki za wananchi wa Iran kama zilivyoainishwa katika pendekezo la vipengele 14”.

    “Kadri wanavyoendelea kuchelewesha, ndivyo walipa kodi wa Marekani watakavyozidi kulipa gharama kubwa,” alisema.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la Tasnim la Iran, pendekezo la Tehran linajumuisha kusitishwa mara moja kwa vita katika maeneo yote ya mapigano, hatua inayorejelea mashambulizi yanayoendelea ya Israel dhidi ya Hezbollah nchini Lebanon, kuondolewa kwa mzingiro wa majini wa Marekani dhidi ya bandari za Iran pamoja na dhamana ya kutofanyika tena kwa mashambulizi dhidi ya Iran.

    Trump aliikosoa vikali ofa hiyo kupitia mtandao wake wa Truth Social akisema: “Nimesoma majibu kutoka kwa wanaojiita ‘wawakilishi’ wa Iran. Siyapendi kabisa, hayakubaliki kabisa.”

    Akijibu kauli hizo, Baghaei alisema Iran itachukua hatua “kwa njia yoyote itakayohitajika kulinda maslahi yake”.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Hujambo na karibu katika matangazo ya moja kwa moja ya Jumanne ya tarehe 12/05/2026.