Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Iran yajibu pendekezo la Marekani la kusitisha vita kupitia Pakistan

Iran inasema imetuma majibu yake kwa "pendekezo la hivi punde la Marekani la kusitisha vita" kupitia Pakistan

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Beldeen Waliaula

  1. Habari za hivi punde, Iran yazionya Uingereza na Ufaransa kuhusu kupeleka wanajeshi katika mlango wa bahari wa Hormuz

    Iran ilizionya Ufaransa na Uingereza kwamba kutumwa kwa vikosi vyao katika Mlango-Bahari wa Hormuz kutakabiliwa na jibu la haraka la Iran.

    Katika siku za hivi karibuni, Ufaransa na Uingereza zimetangaza kupeleka meli za kivita kwenye Mlango wa bahari wa Hormuz.

    Nchi za Ulaya zinasema kutumwa kwa vikosi hivi kunalenga kushiriki katika ujumbe wa kimataifa ili kuhakikisha usalama wa meli katika Mlango wa Hormuz.

    Nchi hizo mbili zinasema ujumbe huo utaanza baada ya kumalizika kwa vita.

    Mvutano kuhusu usalama wa njia hiyo ya maji umeongezeka katika wiki za hivi karibuni baada ya Iran kufunga mlango wa bahari wa Hormuz.

    Tehran hapo awali ilionya kwamba ingezingatia uwepo wowote wa kijeshi wa kigeni karibu na njia ya maji kama "kitendo cha uhasama."

  2. Hapa ndipo tunatamatisha matangazo yetu ya moja kwa moja. Kwaheri.

  3. "Hatujamaliza oparesheni yetu dhidi ya Iran" - Trump

    Donald Trump ameiambia televisheni ya Marekani ya ABC kuwa hakusema wamemaliza oparesheni ya kijeshi nchini Iran ila wameweza kuishinda kivita

    Rais huyo aliongezea kuwa “hatuwezi kuiruhusu Iran kuwa na silaha za nyuklia kwa sababu ni watu wenye misimamo hatari. Hatuwezi kuwaruhusu wapate uwezo wa nyuklia.”

    Trump aliulizwa kama operesheni za kivita dhidi ya Iran zimekamilika na akafafanua kuwa “Sikusema hivyo. Nilisema tumewashinda, lakini hiyo haimaanishi kuwa kila kitu kimeisha. Tunaweza kuendelea kwa wiki nyingine mbili na kushambulia malengo yoyote. Kuna malengo maalum ambayo huenda tayari tumeyashambulia kwa asilimia 70, lakini bado kuna mengine tunayoweza kulenga.”

    Trump alisema kuwa hata kama Marekani haitafanya mashambulizi zaidi, Iran itahitaji miaka mingi ili kujijenga upya.

  4. Waziri mkuu wa Qatar: Pande zote mbili lazima zishirikiane kumaliza vita

    Waziri Mkuu wa Qatar amefanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya kigeni wa Marekani kuhusu kumaliza vita vya Marekani dhidi ya Iran.

    Katika taarifa iliyotolewa na serikali ya Qatar, Waziri Mkuu na Waziri wa mkuu wa Qatar, Mohammed bin Abdulrahman Al Thani, katika mkutano na Marco Rubio mjini Miami, alitaka pande hizo mbili zinazozozana, kuelekeza nguvu zao katika kumaliza vita na “kushughulikia chanzo cha mgogoro huo kwa njia ya amani.”

    Kulingana na taarifa hiyo, Qatar inataka “makubaliano ya kina” yatakayohakikisha kuna amani ya kudumu eneo hilo la Mashariki ya Kati.

    Saa chache baada ya Mohammed bin Abdulrahman Al Thani kukutana na Waziri wa Mambo ya kigeni wa Marekani, pia alizungumza kwa simu na Waziri wa Mambo ya kigeni wa Iran Abbas Araqchi.

    Shirika la habari la serikali ya Iran, IRNA, limechapisha kuwa katika mazungumzo hayo ya simu walijadili kuhusu “hali ya sasa ya eneo hilo na mwenendo wa kidiplomasia,” lakini halikutoa maelezo zaidi.

    Pia unaweza kusoma:

  5. "Uvumilivu wetu unaisha hii leo" - Iran

    Vyombo vya habari vya Iran vinasema kamanda wa kambi ya Khatam al-Anbiya amekutana na kiongozi mkuu wa taifa hilo Mojtaba Khamenei.

    Vyombo hivyo, bila kuchapisha picha zozote, vilisema kuwa kamanda huyo alimpa Khamenei “taarifa kuhusu maandalizi ya vikosi vya kijeshi vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ikiwemo Jeshi la Iran, Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC), polisi wa mipakani, na kikosi cha Basij.”

    Kulingana na ripoti hizo, Kiongozi wa Jamhuri ya Kiislamu aliwashukuru wanajeshi wa Iran kwa kupigana vita dhidi ya Marekani na Israel na “ametangaza hatua mpya pamoja na mbinu za kukabiliana na maadui.”

    Aidha msemaji wa Kamati ya Usalama wa Taifa na Sera za Kigeni katika Bunge la Iran amesema kuwa “uvumilivu na kujizuia ” kwao utaisha hii leo.

    Ebrahim Rezaei aliandika kwenye mtandao wa X, kuwa “Shambulio lolote dhidi ya meli zetu litakabiliwa na jibu kali kutoka Iran na tutalenga meli na kambi za Marekani.”

    Rezaei aliongozea kuwa “Lazima muzoee utaratibu huu mpya wa kikanda.”

    Pia unaweza kusoma:

  6. Habari za hivi punde, Iran yasema imetoa majibu yake kuhusu pendekezo la Marekani kusitisha vita

    Iran inasema imetuma majibu yake kwa "pendekezo la hivi punde la Marekani la kusitisha vita" kwa Pakistan leo.

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema kwamba itajibu pendekezo la Marekani "baada ya kukamilisha uchunguzi na hitimisho la mwisho."

    Kwa mujibu wa ripoti za vyombo vya habari vya Iran, lengo kuu la jibu kwa pendekezo hilo la Marekani ni "kukomesha vita na usalama wa baharini katika Ghuba ya Uajemi na Mlango Bahari wa Hormuz."

    Marekani ilitoa ofa nyingine kwa Iran wiki iliyopita, na Donald Trump amesema mara kadhaa tangu wakati huo kwamba anasubiri majibu ya Tehran.

    Kulingana na vyombo vya habari vya Marekani mpango wa hivi karibuni kutoka kwa utawala wa Donald Trump ni pendekezo la ukurasa mmoja na aya 14.

  7. Nairobi kuwa mwenyeji wa mkutano wa Africa Foward Summit 2026

    Kenya inatarajiwa kuwa mwenyeji wa kongamano la kimataifa la Africa Forwad Summit 2026.

    Mkutano huu utawaleta pamoja zaidi ya viongozi wa kitaifa 30,wawakilishi 4,000, wanabiashara mashuhuri 2,500, wawekazaji, mashirika yasiyo ya kiserikali na washirika wengine kutoka bara Afrika na jumuiya ya kimataifa.

    Mkutano huo wa siku mbili utakao ongozwa na Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron na Rais wa Kenya William Ruto utafanyika katika ukumbi wa KICC jijini Nairobi.

    Mkutano huu unatarajiwa kuimarisha uhusiano wa Ufaransa na Afrika katika sekta ya uwekezaji na uvumbuzi mbalimbali.

    Marais mbali mbali ikiwemo rais wa Sierra Leone Julius Maada Bio, tayari wamewasili jijini Nairobi, huku usalama ukiimarishwa katika mji huo mkuu wa Kenya.

    Barabara kuu za mji huo pia zinatarajiwa kufungwa siku ya Jumatatu na Jumanne.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Nchi zitakazotekeleza vikwazo vya Marekani zitapata ugumu kupita Mlango bahari wa Hormuz

    Jeshi la Iran limesema kuwa nchi zitakazotekeleza vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran, zitapata ugumu kupita katika Mlango bahari wa Hormuz.

    Msemaji wa jeshi la Iran amesema kuwa, “Kuanzia sasa, nchi ambazo zitafuata maelekezo ya Marekani katika kuweka vikwazo dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran zitakumbana na changamoto ya kupita katika Mlango bahari wa Hormuz.”

    Kulingana na shirika la habari la serikali ya Iran, IRNA, msemaji wa jeshi Mohammad Akraminia alisema kuwa “Wamarekani hawataweza kugeuza eneo hili la kaskazini mwa Bahari ya Hindi kuwa kizuizi halisi na meli zao za kijeshi.”

    Msemaji huyo aliongezea kuwa “bila shaka, madai ya kizuizi yalikuwa jaribio la kutumia propaganda ili kudhoofisha usimamizi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Mlango bahari wa Hormuz,”

    Aidha aliongezea kuwa “Biashara yetu ya baharini inaendelea kama kawaida, ni meli chache tu zimezuiliwa, huku sisi pia tukuzuia meli za utawala wa Kizayuni”

    Pia unaweza kusoma:

  9. Habari za hivi punde, Meli ya Marekani yashambuliwa pwani ya Qatar - Fars

    Shirika la Habari la Fars, likinukuu "chanzo cha habari," limesema kwamba meli hiyo kubwa iliyolengwa karibu na pwani ya Qatar ilikuwa ya Marekani na "ilikuwa ikipepea chini ya bendera ya Marekani.

    Mtandao wa Habari wa Iran pia umenukuu duru za habari zikisema kuwa meli ya mizigo iliyokuwa ikilengwa ilikuwa ikisafiri chini ya bendera ya Marekani na ni ya Marekani.

    Marekani haijatoa maoni yoyote.

    Kamandi ya Operesheni za Baharini ya Uingereza iliripoti saa chache zilizopita kwamba meli ilishambuliwa na "kombora lisilojulikana" kilomita 43 kaskazini mashariki mwa Doha, mji mkuu wa Qatar, na moto mdogo ukazuka.

  10. India yafanyia majaribio kombora jipya lenye uwezo wa kurusha makombora mengi kwa wakati mmoja

    Jeshi la India limefanyia majaribio kizazi kipya cha makombora ya hali ya juu ya Agni kwenye pwani ya Odisha.

    Kombora hili linaweza kurusha makombora mengi katika maeneo tofauti.

    Kulingana na Wizara ya Ulinzi ya India, mfumo huu wa makombora ulijaribiwa mnamo Ijumaa, Mei 8.

    "India mnamo Mei 8 ilifanikiwa kujaribu kombora la hali ya juu la Agni lenye mfumo wa MIRV kutoka Kisiwa cha Abdul Kalam, Odisha," Wizara ya Ulinzi ilisema katika taarifa.

    Taarifa hiyo iliendelea kwa kusema kuwa kombora hilo lenye vichwa vingi vya kivita, lililenga maeneo kadhaa yaliyotengwa katika eneo pana la kijiografia katika Bahari ya Hindi.

    Uzalishaji wa makombora ya Agni ulianza nchini India mwaka 1983. Kizazi kilichopita (cha tano) Agni ni balestiki nunayoweza kusafiri kutoka bara moja hadi jingine pamoja na kuwa na uwezo wa kubeba kichwa cha nyuklia, mbali na kwamba kombora hilo linaweza kusafiri umbali wa kilomita 5,000.

  11. Jeshi la Israel latangaza kuwaua zaidi ya wapiganaji 10 wa Hezbollah

    Wizara ya Afya nchini Lebanon imetangaza kuwa idadi ya vifo inayotokana na mashambulizi ya Israel yaliyofanyika hapo jan imefikia watu 39.

    Kulingana na wizara hiyo moja ya mashambulizi ya Israel katika mji wa Saskia kusini mwa Lebanon ilisababisha vifo vya watu saba, akiwemo mtoto mmoja.

    Jeshi la Israel lilisema mashambulizi hayo yalilenga wapiganaji wa Hezbollah, na kuongezea kuwa “linafahamu kuhusu vifo vya raia.”

    Tangu Rais wa Marekani Donald Trump kutangaza makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya serikali ya Israel na Lebanon mwezi Aprili tarehe 16, mashambulizi na mapigano kati ya jeshi la Israel na Hezbollah bado yanaendelea.

    Jeshi la Israel lilisema hii leo kuwa vikosi vyake vimewaua zaidi ya wapiganaji 10 wa Hezbollah na kushambulia takriban maeneo 40 na kuharibu miundombinu ya kundi hilo katika saa 24 zilizopita.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Putin asema vita vya Urusi na Ukraine viko karibu kumalizika

    Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema kuwa anaamini vita vya Ukraine vinaeleka kufika tamati,alitoa kauli hiyo saa chache tu baada ya kusema atashinda vita nchini Ukraine wakati wa gwaride la Siku ya Ushindi mjini Moscow.

    “Nadhani suala hili linaelekea kuisha,” Putin aliwaambia waandishi wa habari kuhusu vita vya Urusi na Ukraine, ambavyo ni vita vibaya kuwahi kushuhudiwa bara Ulaya tangu Vita vya Pili vya Dunia.

    Aidha Putin aliongezea kuwa yuko tayari kujadili mipango mipya ya usalama bara Ulaya, na kupendekeza kuwa mshirika wake katika mazungumzo hayo atakuwa Kansela wa zamani wa Ujerumani Gerhard Schröder.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Meli ya watalii iliyokumbwa na mlipuko wa virusi vya Hantavirus yawasili Tenerife

    Takriban mwezi mmoja baada ya abiria wa kwanza kufariki kutokana na virusi vya hantavirus akiwa ndani ya meli ya watalii ya MV Hondius, meli hiyo imewasili Tenerife katika Visiwa vya Canary.

    Maandalizi makubwa yamekuwa yakiendelea ili kuipokea meli hiyo katika bandari ya Granadilla na kusaidia zaidi ya watu 100 kurejeshwa makwao.

    Meli ya Hondius haijaruhusiwa kufika bandarini, lakini imesalia eneo salama baharini karibu na kisiwa hicho, ili iendelee kubaki katika hali ya kutengwa ili kuzuia maambukizi kwa wananchi wa kawaida wa Hispania.

    Pia unaweza kusoma:

  14. Iran yaonya kushambulia vituo vya kijeshi vya Marekani na meli za adui iwapo meli zao mafuta zitalengwa

    Jeshi la Iran (IRGC) limetishia kulenga maeneo ya Marekani iwapo meli za mafuta za Iran zitashambuliwa, huku Washington ikiwa bado inasubiri majibu ya Tehran kuhusu pendekezo lake la hivi karibuni la mazungumzo.

    Katika taarifa iliyotolewa hapo jana, siku moja tu baada ya Marekani kushambulia meli mbili za mafuta za Iran katika Ghuba ya Oman, Iran imesema kwamba “shambulio lolote dhidi ya meli za mafuta na meli za kibiashara za Iran, zitawafanya washambulie vituo vya kijeshi vya Marekani Pamoja na meli za adui"

    Pia unaweza kusoma:

  15. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja.