Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Siri ya 'nyumba ya Mojtaba Khamenei'
Wiki iliyopita, maadhimisho ya siku ya 40 tangu mazishi ya Ali Khamenei yalifanyika Tehran, Qom, na Mashhad. Kama ilivyokuwa wakati wa mazishi na uzikaji, Mojtaba Khamenei hakuwepo katika mfululizo huu mpya wa sherehe, au hakuna picha wala sauti yake iliyotolewa.
Safari hii, tofauti na wakati wa mazishi, inaonekana hakukuwa na matarajio makubwa ya umma kuhusu kuwepo kwa kiongozi wa tatu wa Jamhuri ya Kiislamu; kana kwamba kuendelea kwake kujificha hakukuibua tena hisia kali katika vyombo vya habari kama ilivyokuwa hapo awali.
Hoja kuu inayotolewa na wasemaji wa serikali kuhalalisha kutokuwepo huku ni masuala ya kiusalama. Mtazamo mkuu wa wasemaji hawa ni kwamba kutoa video ya kiongozi huyo mpya kungeweza kufichua mahali alipo na kuhatarisha maisha yake.
Katika kujibu utata kuhusu sababu ya kutotolewa hata kipande kidogo cha sauti ya Mojtaba Khamenei, vyombo vya habari vya serikali vinadai kuwa hata sauti yake inaweza kufichua mahali alipo.
Ni kweli kwamba kwa kuchunguza kwa makini faili la sauti, inawezekana kupata taarifa muhimu kama vile sifa za vifaa vya kurekodia, sifa za mfumo wa umeme, au baadhi ya sifa za kimwili na kimazingira za eneo la kurekodia.
Lakini ikiwa sababu kuu ya kuficha picha na sauti ya kiongozi huyo ilikuwa masuala ya kiusalama, kulikuwa na njia za kushughulikia hatari zinazoweza kujitokeza.
Kwa mfano, taasisi za serikali zingeweza kuepuka kabisa kutumia zana za kompyuta kurekodi sauti ya Mojtaba Khamenei na badala yake kutumia vifaa vya enzi za kabla ya teknolojia ya kidijitali, kama vile kanda za kaseti na virekodi sauti vya zamani.
Vilevile, ili kuzuia kufichuliwa kwa sifa za kimwili na kimazingira za eneo la kurekodia, ilikuwa inawezekana kurekodi sauti katika mazingira yenye vipimo na hali tofauti kabisa na makazi ya kawaida ya kiongozi huyo, na kisha sauti hiyo, kwa mfano, kanda iliyorekodiwa, ingeweza kuchezwa kwa wasikilizaji kutoka eneo la mbali.
Katika mazingira hayo, madai ya vyombo rasmi vya habari kwamba sababu ya kutotoa picha au sauti ya Mojtaba Khamenei ilikuwa hofu ya kiusalama, kwa wazi hayajawashawishi watu wengi. Jitihada za maafisa wa serikali kutoa maelezo zaidi kuhusu hofu hizo za kiusalama zimesababisha tu kuchapishwa kwa simulizi zisizo za kawaida zaidi.
Kwa mfano, Salar Velayatmadar, mjumbe wa Tume ya Usalama wa Taifa ya Bunge, aliona kuwa kutotolewa hadharani kwa sauti na picha ya Kiongozi huyo kulifuata "maoni ya wanazuoni wa Najaf, Qom, na Mashhad pamoja na uamuzi wa maafisa wa usalama," ili "maadui wasiweze kumdhuru kupitia njia maalum na sayansi za ajabu zinazojadiliwa katika vyuo vikuu kama vile Chuo Kikuu cha Sayansi za Ajabu cha Tel Aviv."
End of Pia unaweza kusoma
"Iwapo kiongozi atashindwa kutekeleza majukumu yake kutokana na ugonjwa au ajali"
Mazingira yanayotokana na kauli za serikali zinazohusisha kutokuwepo kwa Mojtaba Khamenei na masuala ya kiusalama yamesababisha sehemu ya umma kuhitimisha kuwa huenda hayuko hai au alijeruhiwa vibaya wakati wa shambulio dhidi ya makazi yake.
Tathmini zilizochapishwa, zikinukuu vyanzo vya Marekani na Israel, kwa kiasi kikubwa zimesisitiza dhana kwamba Mojtaba Khamenei alinusurika shambulio hilo lakini alipata majeraha makubwa.
Vyombo kadhaa vikubwa vya habari vya kimataifa vinaonekana kukubaliana kwa kiasi fulani na dhana hii.
Katika muktadha huu, imeimarika zaidi dhana kwamba huenda mlipuko huo uliathiri kwa kiasi kinachoonekana muonekano na labda uwezo wa kuzungumza wa Mojtaba Khamenei; athari ambazo, angalau hadi sasa, imekuwa kwa maslahi ya serikali kuzificha.
Ni muhimu kuzingatia kwamba kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Kiislamu, iwapo "kiongozi atashindwa kutekeleza majukumu yake ya kisheria" au "ikibainika kuwa hakukidhi vigezo fulani tangu awali," hastahiki kuendelea na wadhifa huo.
Zaidi ya hayo, iwapo "kiongozi atashindwa kwa muda kutekeleza majukumu yake ya uongozi kutokana na ugonjwa au ajali nyingine," majukumu yake yatachukuliwa na baraza linaloundwa na rais, mkuu wa idara ya mahakama, na mmoja wa wataalamu wa sheria za Kiislamu kutoka Baraza la Walinzi (Guardian Council) ambaye atachaguliwa na Baraza la Uamuzi wa Maslahi ya Taifa (Expediency Discernment Council)hadi hapo atakapopona.
Bila shaka, haionekani kuwa hata kama wangekuwa na uhakika kuhusu hali mbaya ya kimwili ya Khamenei, wajumbe wa Baraza la Wataalamu (Assembly of Experts) wangekuwa na nia au uwezo wa kuhoji uongozi wake.
Hata hivyo, katika kipindi cha baada ya Ali Khamenei, kudhibiti jambo lolote linaloweza kudhoofisha nafasi ya kiongozi mpya ilikuwa kipaumbele kikubwa kwa serikali ya Iran.
Hii ilikuwa kweli hasa katika hali ambapo, mbali na masuala ya kisheria, kuona picha ya kiongozi au kusikia sauti yake akiwa katika hali isiyoridhisha kungeweza kuimarisha "hisia ya kutokuwa na utulivu" miongoni mwa wafuasi wa serikali.
Kuhusiana na umuhimu wa hisia kama hiyo, haitakuwa jambo lisilofaa kukumbushia simulizi ya daktari wa Ruhollah Khomeini (Hassan Arefi) kwamba baada ya kuthibitika kuwa kiongozi huyo wa wakati huo alikuwa na saratani iliyoendelea, kundi la maafisa lilipinga vikali matibabu yake ya kemotherapi, kwa kuwa walikuwa na wasiwasi kuhusu athari mbaya ambazo "muonekano wake bila ndevu" ungeweza kuwa nazo kwa maoni ya umma.
Labda ni katika muktadha huu ambapo kauli za hivi karibuni za msemaji wa wizara ya afya zinapaswa kutazamwa; msemaji huyo alisisitiza kuwa kiongozi mpya alikuwa amejeruhiwa lakini majeraha yake hayakuwa "makubwa kiasi cha kuharibu sura yake."
Hossein Kermanpour, anayedai kumuona Khamenei hospitalini kabla hajateuliwa kuwa kiongozi, alisema yeye na wenzake walikuwa na wasiwasi kuhusu "jinsi ya kujenga simulizi" baada ya mtu huyo kupelekwa hospitalini, ingawa alikiri kuwa "hajui ni watu wangapi watakaoamini anachosema."
Kuchapishwa mara kwa mara kwa picha ghushi za kiongozi huyo wa tatu kwenye mitandao ya kijamii na vyombo rasmi vya habari ili kuthibitisha "afya" yake, nako kunapaswa kutathminiwa katika muktadha huu.
Wiki iliyopita tu, wakati huo huo amri zilipotolewa za kuwateua makamanda wa ngazi ya juu wa IRGC na Basij, vyombo vingi rasmi vya habari vya Iran vilichapisha picha iliyoitwa "Muonekano Mpya" wa Mojtaba Khamenei, ambayo baadaye ilibainika haraka kuwa ni toleo lililorekebishwa la picha ya zamani.
"Uongozi" katika mazingira mapya
Kukubali kuwa kutokuwepo kwa Mojtaba Khamenei katika nyanja ya umma kunatokana na matatizo ya kiafya kunaimarisha dhana fulani: kwamba nafasi ya juu kabisa serikalini inahitaji, kwa kiwango kisicho na kifani, kundi la watu wanaohusika na kumhudumia na kumtunza muda wote, jambo ambalo katika nyaraka rasmi huitwa "nyumba ya uongozi."
Kwa vitendo, dhana hiyo inamaanisha kuwa watu hawa wa karibu wamekuwa na mawasiliano ya mara kwa mara na kiongozi huyo; hii ni licha ya ukweli kwamba hata rais amedai kukutana na Mojtaba Khamenei mara mbili tu tangu kuteuliwa kwake kuwa kiongozi, huku maafisa wengine wakiwa hawajatoa madai kama hayo.
Hata hivyo, muda mfupi baada ya Masoud Pezeshkian kuelezea kwa mara ya kwanza kukutana na Mojtaba Khamenei, baadhi ya vyombo vya habari vya Iran vilidai kuwa Ali Abdollahi, aliyekuwa kamanda wa Makao Makuu ya Kati ya Khatam al-Anbia wakati huo, naye alikutana naye, ingawa kamanda huyo mwenyewe hajazungumzia mkutano huo.
Kwa upande mwingine, ni muhimu kuzingatia kwamba kutokuwepo kwa Kiongozi huyo hadharani au mashaka kuhusu hali yake ya kiafya, angalau hadi sasa, hakujafanya "hali yake ya kawaida" (status quo) na jumbe zinazochapishwa kwa jina lake kupoteza umuhimu au uhalali.
Mfano mmoja unaoibua tafakari kuhusu ushawishi huu ulikuwa ni kutolewa kwa ujumbe uliohusishwa na Kiongozi huyo kufuatia kuidhinishwa kwa hati ya makubaliano kati ya Iran na Marekani na Baraza Kuu la Usalama wa Taifa, kwa wingi wa kura 12 kati ya wajumbe 13 waliokuwepo kwenye mkutano wa baraza hilo.
Ujumbe huo ulionyesha kuwa Mojtaba Khamenei alikuwa na maoni tofauti "kimsingi" kuhusu hati hiyo ya makubaliano; jambo hili liliwafanya wale walioiidhinisha, kuanzia makamanda wa ngazi ya juu wa jeshi hadi viongozi wa mihimili mitatu ya serikali, kukabiliwa na shinikizo kubwa kutoka kwa wapinzani wa mazungumzo na Marekani.
Hali ilifikia hatua ambapo Masoud Pezeshkian alipokea vitisho vya kuuawa hadharani, na Shirika la Habari la Fars ambalo lina uhusiano na shirika la Basij likatoa filamu ya makala yenye kichwa "Mapinduzi ya Qalibaf" (Qalibaf's Coup).
Utambulisho usiojulikana wa "mzunguko wa watu wanaoaminika"
Hakuna makadirio ya uhakika kuhusu muda ambao hadithi ya uwepo wa kiongozi wa tatu wa Jamhuri ya Kiislamu nyuma ya pazia itaendelea.
Lakini ikiwa Mojtaba Khamenei yuko hai, hadi sasa sehemu muhimu ya mfumo wake wa uongozi imetegemea watu wa karibu wanaoaminika ambao utambulisho wao haujulikani, isipokuwa kwa uvumi usio rasmi.
Kuathiri mlinganyo wa serikali kupitia mahusiano ya nyuma ya pazia ni jambo la kawaida kwa viongozi wa zamani wa Jamhuri ya Kiislamu, hasa kiongozi wa pili.
Njia hii, kwa kuzingatia taarifa zilizopo kuhusu historia ya Khamenei, pia inaendana sana na mwenendo wake wa kisiasa wa huko nyuma. Hii inajumuisha uzoefu kama vile kuongoza baraza la siri la watu watano ambalo, kulingana na Mohammad Sarafraz (mjumbe wa zamani wa baraza hilo), lilifanya maamuzi ya nyuma ya pazia kuhusu masuala nyeti ya kisiasa na kiusalama kwa zaidi ya miongo miwili.
Licha ya hayo yote, inaonekana kuwa tangu kutangazwa kwa uongozi wa Mojtaba Khamenei, tunashuhudia kiwango kipya cha "utawala wa nyuma ya pazia," jambo ambalo halijazoeleka hata katika muktadha wa historia ya Jamhuri ya Kiislamu inayojulikana kwa kutokuwa wazi.