Donald Trump amesema kuwa Urusi na Ukraine zitasitisha mapigano kwa siku tatu
Donald Trump ametangaza usitishaji wa mapigano wa siku tatu kati ya Urusi na Ukraine, baada ya nchi hizo mbili kushutumiana kwa kukiuka usitishaji wa mapigano uliotangazwa na kila upande kwa ajili ya maadhimisho ya ushindi wa Umoja wa Kisovieti dhidi ya Ujerumani ya Nazi.
“Usitishaji huu wa mapigano utahusisha kusimamishwa kwa shughuli zote za kivita, pamoja na kubadilishana wafungwa 1,000 kutoka kila nchi,” rais huyo wa Marekani alisema.
Muda mfupi baadaye, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy alithibitisha ushiriki wa Ukraine katika makubaliano hayo, huku vyombo vya habari vya serikali ya Urusi vikisema kuwa Urusi pia imekubali pendekezo hilo.
Awali, pande zote mbili zilidai kuwa upande mwingine uliendelea kushambulia maeneo yao, na meya wa Moscow alisema mji huo ulikuwa umelengwa na mashambulizi ya ndege zisizo na rubani usiku kucha.
Katika ujumbe wake, Trump alisema aliomba binafsi usitishaji huo wa mapigano wa siku tatu na “anathamini sana kukubaliwa kwake na Rais Vladimir Putin pamoja na Rais Volodymyr Zelenskyy.”
Putin alikuwa ametangaza usitishaji wa mapigano kwa tarehe 8 hadi 9 Mei kabla ya maadhimisho ya Siku ya Ushindi yaliyopangwa kufanyika Jumamosi. Kyiv hapo awali ilikuwa imetoa wito wa usitishaji wa mapigano usio na kikomo kuanzia tarehe 6 Mei.
Urusi imeionya Ukraine kutofanya jaribio lolote la kushambulia gwaride la Siku ya Ushindi litakalofanyika katika Red Square mjini Moscow.
Wizara ya ulinzi ya Urusi imetishia kufanya “shambulio kubwa la kulipiza kisasi kwa makombora” katikati mwa mji wa Kyiv ikiwa Moscow itashambuliwa. Pia imewaonya wanadiplomasia wa kigeni kuondoka katika mji mkuu wa Ukraine kabla ya tarehe 9 Mei.
Unaweza kusoma;