Vyombo vya habari vya Israel vyamkosoa Trump kwa kumtaka kujizuia kufanya mashambulizi

Chanzo cha picha, Jim WATSON / AFP via Getty Images
Vyombo vya habari vya Israel vimemkosoa Rais wa Marekani Donald Trump kwa kuitaka Israel kutofanya mashambulizi dhidi ya Iran, huku Israel ikiendelea kushambulia Iran licha ya wito huo.
Baadhi ya wachambuzi wanaona tofauti hizi za hadharani kuwa sehemu ya mkakati mgumu wa kusimamia mvutano huo.
Tarehe 7 Juni, Israel ililenga makao makuu ya Hezbollah katika kitongoji cha Beirut, hatua iliyosababisha Iran kurusha makombora dhidi ya Israel na kisha Israel kujibu mashambulizi hayo.
Gazeti la kiliberali la Haaretz liliripoti kwamba Israel ilishambulia Iran “licha ya ombi la Trump kwa Netanyahu.”
Ingawa Israel na Iran wameepuka mashambulizi ya moja kwa moja dhidi ya kila mmoja tangu mwanzoni mwa Aprili, Benjamin Netanyahu amekuwa akisisitiza mara kwa mara haja ya kurejea kwenye mzozo, jambo linaloibua swali iwapo makubaliano kati ya Marekani na Iran yanaweza kuzuia kikamilifu mpango wa nyuklia wa Iran na pia kutimiza matarajio ya Israel.
Barak Ravid, mwandishi wa masuala ya kidiplomasia wa Channel 12, alimnukuu afisa mwandamizi wa Marekani na chanzo cha Israel wakisema kwamba Trump alimwambia Netanyahu katika simu: “Usijibu mashambulizi ya makombora ya Iran na ipe diplomasia siku kadhaa zaidi.”
Gazeti la Haaretz liliandika kwamba: “Asubuhi ya leo ilibainika wazi kuwa juhudi hizo zimeshindwa na kwamba Israel imeishambulia Iran,” likiongeza kwamba pia kombora la balistiki lilirushwa kutoka Yemen.
Gazeti la Ma’ariv lilitangaza kwamba Israel ina haki ya kujilinda “kwa nguvu, kwa uthabiti na bila kusita” dhidi ya mashambulizi ya makombora ya Iran, huku likikosoa taarifa kwamba Donald Trump alijaribu kuizuia Israel kujibu mashambulizi hayo. Gazeti hilo liliongeza kuwa Marekani inapaswa kuunga mkono hatua za Israel katika mzozo wa pamoja, badala ya kuzuia hatua hizo.
Unaweza kusoma;












