Awaua wanafamilia sita kabla ya kujiua mwenyewe, polisi wanasema

Chanzo cha picha, Getty Images
Mwanafamilia aliyekuwa na bunduki amewaua watu sita wa familia yake, kisha akajiua, katika shambulizi lililohusisha mfululizo wa ufyatuaji risasi siku ya Jumatatu katika jiji la Muscatine mashariki mwa Iowa, mji ulioko ufukweni mwa mto Mississippi kutoka Illinois, polisi wamesema.
Uchunguzi wa awali kuhusu vurugu za bunduki ulionyesha kuwa ufyatuaji risasi "ulitokana na mzozo wa ndani," Idara ya Polisi ya Muscatine ilisema katika taarifa, ingawa hakuna kilichotajwa haswa kuhusu kile ambacho huenda kilisababisha umwagaji damu.
Wanne kati ya waathiriwa walipatikana wakiwa wamepigwa risasi hadi kufa ndani ya makazi kulingsna na maafisa wa polisi wakijibu ripoti za kwanza za milio ya risasi muda mfupi baada ya saa sita mchana kwa saa za eneo.
Ingawa mshukiwa wa muuaji alikuwa ametoroka eneo la tukio kabla ya maafisa kufika, alitambuliwa haraka kama Ryan Willis McFarland, 52, wa Muscatine, na alikuwa kwenye njia ya mji karibu na daraja la watembea kwa miguu, Mkuu wa Polisi Anthony Kies alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari.
Wakati maafisa walipokuwa wakizungumza naye, alijiua, polisi walisema.
Baada ya taarifa kuibuka zikionyesha kuwa huenda kulikuwa na waathiriwa wengine, polisi walipata miili ya watu wengine wawili ambao McFarland aliaminika kuwapiga risasi - mmoja katika nyumba iliyo karibu na mwingine katika biashara.
Waathiriwa wote waliaminika kuwa wanafamilia wa mshambuliaji huyo, Kies alisema. Hawakutambuliwa hadharani na inasemekana kuwa takriban wawili kati ya waathiriwa walikuwa watoto.
Mkuu wa polisi aliwaambia waandishi wa habari kwamba McFarland alikuwa na rekodi ya uhalifu hapo awali lakini alikataa kufafanua.
Soma zaidi:


